NA MWANDISHI WETU,MBEYA
NAIBU Waziri wa Kilimo David Silinde amepokea na kumkabidhi Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Homera mbolea ya ruzuku ya NPK 10:18:24 tani 61,000 itakayotumika katika kilimo cha zao la tumbaku
Mbolea hiyo imekabidhiwa kwa uongozi wa mkoa ili ianze kusambazwa kwa wakulima wote nchini
Akizungumza Septemba 19,2024 mara baada ya kukabidhi mbolea hiyo katika ghala la Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) lililopo Kata ya Iyunga, Jijini Mbeya, Silinde ameeleza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan alielekeza katika msimu huu wa kilimo unaoanza mbolea za ruzuku ziwafikie wakulima kwa wakati kabla mvua hazijaanza kunyesha, hivyo maelekezo hayo yametekelezwa
“Natumia fursa hii kuwajulisha Watanzania kuwa mbolea ya ruzuku imeanza kuingia nchini hususani wakulima wa zao la tumbaku,nitaikabidhi kwa Mkuu wa Mkoa ili iwe mahali salama naye kuhakikisha inawafikia wakulima kwa wakati kwa kuwa wakuu wa mikoa ndio wasimamizi wakuu wa kilimo katika Mamlaka za Serikali za Mitaa,”ameeleza Silinde
Akipokea mbolea hiyo Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Homera amesema hitaji la muda mrefu la wananchi wa Wilaya ya Chunya na Mkoa wa jirani wa Songwe juu ya kuwezeshwa mbolea ya ruzuku kwa ajili ya zao la tumbaku,Rais Dkt. Samia Samia Suluhu Hassan amewajibu wananchi hao kwa vitendo.
Amesema Rais Dkt.Samia amewajibu wananchi hao kwa kuleta magari yenye shehena ya mbolea ambapo mpaka sasa takribani magari zaidi ya 170 kati ya magari 2030 yameshafika.
“Kwa mbolea hii tunakwenda kuzalisha tani zaidi ya 30,000 za tumbaku kwa msimu unaoanza wa kilimo.
‘’Tumetoka kwenye tani 8,000 tukaja tani 16,000 na sasa tupo tani 24,000 na dhamira yetu ni kuzalisha tani 30,000 mpaka tani 40,000 kwa zao la tumbaku ndani ya Mkoa wa Mbeya na mkoa wa jirani wa Songwe,”amefafanuwa Homera
Aidha amebainisha kuwa dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi wanaondokana na umaskini hivyo kuwataka viongozi wa vyama vya ushirika kufika katika ghala hilo kwa wakati ili kuchukua na kusambaza mbolea hiyo.

Akieleza malengo ya Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC), Mkurugenzi Mkuu Samuel Mshote ameeleza kuwa kwa mwaka wa fedha 2024/2025 TFC imepanga kuuza na kusambaza mbolea ya ruzuku tani 130,000 kati ya hizo mbolea ya zao la tumbaku ni tani 61,000.




Discussion about this post