NA MWANDISHI WETU,KILIMANJARO
MIRADI ya Majisafi na Usafi wa Mazingira, pamoja na Chombo cha Watumia Maji imekaguliwa katika Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro ili kuona ubora wake kwa jamii.
Hilo limefanyika kwa wataalamu wa Sekta ya Maji na wawakilishi wa Benki ya Dunia kukagua Mradi wa Uboreshaji Huduma ya Maji Kiruavunjo Kusini na Mradi wa Usafi wa Mazingira katika Zahanati ya Kikalala .
Mradi huo wa Uboreshaji Huduma ya Maji Kiruavunjo Kusini unahudumia wakazi zaidi ya 6000 na kukamilika kwake kutaongeza hali ya upatikanaji wa huduma ya maji kwa asilimia 100.
Aidha, pamoja na hilo lakini pia ukaguzi umefanyika katika Chombo cha Watumia Maji cha Kiruakahe kinachohudumia vijiji 28, ili kuona namna wanavyoweza kutoa huduma kwa wananchi.
Kwa upande wa eneo la Usafi wa Mazingira ukaguzi umefanyika katika Zahanati ya Kikalala ambayo ilipata fedha kwa ajili ya kutengeneza miundombinu ya usafi wa mazingira kiasi cha Sh.Milioni 470.
Mradi wa Usafi wa Mazingira Kikalala umewezesha wakazi wa eneo hilo kuwa na uhakika wa huduma bora za afya na usalama dhidi ya magonjwa yanayosababishwa na uchafu.

Akizungumza wakati wa ukaguzi huo Oktoba 2,2024 katika eneo la mradi huo Kiruavunjo,Meneja wa Wakala wa Majisafi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro Mhandisi Mussa Msangi amesema kwa sasa wananchi wanapata maji kwa asilimia 45 na pindi mradi ukikamilika huduma ya maji itakuwa asilimia 100.
‘’Leo tumetembelea na kujionea mradi huu na chombo cha watumiaji maji,chombo imara imara kinachohudumia vijiji 28 na awali tulikuwa na upungufu wa maji lakini sasa wanatumia maji kwa sababu mradi umefika asilimia 80.
‘’Ndani ya mwezi huu wa 10,2024 wataanza kuongeza maji kiasi cha lita 500020 na walikuwa wanakusanya mapato ya kiasi cha Sh.Milioni 6 na yataongezeka hadi Sh.Milioni 10 na kufanya jumla ya mapato wanayopata kama Jumuiya ya Sh.Milioni 60 kwa mwezi na yatafikia Sh.Milioni 63.
‘’Haya ni mafanikio makubwa sana na itaongeza huduma ya upatikanaji wa maji na watu 15,000 watumiaji wa maji katika wilaya yetu na kutusukuma kutoka asilimia 84.5 hadi asilimia 90.2 itakapofika mwezi Juni 2025’’amesema Mhandisi Msangi

Akizungumzia kuhusu Mradi wa Zahanati ya Kisalala,Mganga Mkuu wa Wilaya ya Moshi Mjini mkoani Kilimanjaro Dkt.Juma Mapokaleo amesema walipokea fedha za mwaka wa fedha 2023/24 kwa ajili ya kutengeneza miundombinu ya Usafi wa Mazingira
‘’Kwa kutekeleza mradi huu tunapata faida ya kuhakikisha taka zote zinazozalishwa kwenye Zahanati zinaweza kuchomwa na kuteketezwa kabisa lakini inazidi kutupa hamasa kwa wananchi ambao tunaowahudumia katika eneo hili kuwa tunatakiwa kujitunza kwa usafi
‘’Baada ya kuwa na vyoo bora na sehemu za kunawia mikono,kabla ya kuanza huduma zetu asubuhi tunawapa elimu ya afya pamoja na kuwasisitiza namna bora ya kutumia miundombinu ya maji safi ili kuweza kujikinga ya magonjwa ya mlipuko na mengine’’amesema Dkt Mapokaleo
Naye mkazi wa Kiruavunjo Hellen Msofe amesema wamefurahi kupata mradi huo wa maji safi kwa kuwa awali walikuwa wakitumia maji ya mtiririko na kusababisha athari za maradhi ya tumbo na kupata matatizo kwa muda mrefu
‘’Lakini kwa sababu Mama Samia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameona kuna umuhimu wa kutusaidia sisi akina mama tunaoishi maeneo haya kwa kutuletea mradi mkubwa wa maji kama huu’’amesema Msofe




Discussion about this post