NA GOODLUCK HONGO
HEROIN ni aina ya dawa ya kulevya inayotengenezwa na kemikali inayoitwa ‘morphine’ ambayo hupatikana kwenye utomvu ‘opium’ wa tunda la mmea wa afyuni‘opium poppy’.
Mmea huo unadaiwa kulimwa zaidi kwenye nchi za Afghanistan ,Mynamar(Burma),Laos na baadhi ya nchi za America Kusini.
Heroin ni mojawapo ya dawa za kulevya zinazoongoza duniani kuwa na watumiaji wengi wanaohitaji tiba na hujulikana kwa majina ya mtaani kama unga,ngada,teli(cocktalil),msharafu,white,kijiwe.mdudu na brown
Kwa mujibu wa taarifa ya Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA) iliyotolewa mwaka 2023 TOLEO NO. 001,inaeleza kuwa sehemu kubwa ya jamii pamoja na wengi wa watumiaji wa heroin hudhani kuwa dawa zote za unga ni cocaine.
Taarifa hiyo inaeleza kuwa heroin inayopatikana huwa katika umbo la mawemawe na husagwa kabla ya kutumika na hutumika kwa wingi zaidi nchini kuliko cocaine.
Hata hivyo madhara ya heroin yanatofautiana na cocain ambapo wengi wa watumiaji wa heroin walianza na kuvuta bangi tofauti na miaka ya nyuma.
Madhara kwa jamii
Heroin inatajwa kuwa na madhara makubwa ikiwemo kiafya,kiuchumi,kijamii ambapo upande wa kijamii,mraibu anaweza kutowajibika na kushindwa kutimiza majukumu shuleni,kazini na familia kunakopelekea kutelekeza wenza na watoto,kutalikina ,kupoteza ajira au kutoajirika pamoja na watoto wa mitaani.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya DCEA hayo yote huleta umasikini kwa familia,jamii na Taifa kwa ujumla.
Heroin huongeza vitendo vya uhalifu vikiwemo wizi,ukabaji,utapeli,utekaji,mauaji na ujangili ambapo pia biashara ya heroin inachochea biashara haramu ya binadamu ambapo vijana wa kitanzania huwekwa rehani nje ya nchi(bondi) kutumikishwa kingono na kuhatarisha maisha yao
Madhara ya kiuchumi
Kwa upande wa kiuchumi,dawa hiyo ya kulevya ya heroin hupunguza nguvu kazi na kuongeza umasikinikwa familia ,jamii na taifa kwa ujumla.
Biashara ya dawa za kulevya husababisha mzunguko wa fedha haramu,mfumuko wa bei,utakatishaji fedha ,kukithiri kwa rushwa na kuongeza tofauti na kipato ambapo pia hiingiza serikali katika kutumia gharama kubwa kdhibiti tatizo la dawa za kulevya kwenye ukamataji,matibabu na kutoa elimu
Madhara ya kiafya
Heroin inasababisha magonjwa mbalimbali kama moyo,mapafu,meno,ngozi,figo na saratani,hupunguza kasi ya utendaji kazi wa mfumo wa fahamu na kuathiri umakini.
Madhara mengine ni pamoja na kukosa hamu ya kula na kudhoofu kiafya,kubadilisha mfumo wa hedhi kwa wanawake,kupunguza nguvu za kiume na kuweza kusababisha ugumba.
Heroin husababisha hali ya mraibu kukosa hamu ya kula na kudhoofu kiafya,kujidunga husababisha mishipa ya damu kusinyaa au kupotea na hivyo kushindwa kupata msaada wa matibabu kwa haraka pale panapohitajika.
Heroin inatajwa kusababisha uraibu wa haraka,vifo vinavyotokana na kuzidisha kiasi cha matumizi ya dawa hizo na mtumiaji anapokosa hupatwa na arosto yenye maumivu makali,homa,kuharisha ,kizunguzungu na kichefuchefu ambayo hudumu kati ya masaa saa 48 hadi 72.
Mazingira duni ya utumiaji na kushirikiana vifaa vya kujidunga huongeza maambukizi ya VVU,homa ya ini na kifua kikuu.
Kutokana na madhara hayo Serikali kupitia DCEA imekuwa ikifanya kazi kubwa ya kuhakikisha kuwa afya za watanzania na vizazi vyao inakuwa salama kwa kuwakamata wauzaji,wasambazaji,wapokeaji na wale wanaohifadhi.
Kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Dawa za Kulevya ya Mwaka 2023 iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu(Sera,Bunge na Uratibu) kupitia Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA) inaeleza ukamataji huo ni mkubwa kuwahi kutokea nchini katika historia ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya tangu nchi ipate uhuru wake.
‘’Takwimu zinaonesha kuwa mwaka 2023 kiasi cha heroin tani 1.31 ambacho ni sawa na kilogram 1,314.28 zilikamatwa,ukamataji huu ni mkubwa kuwahi kutokea tangu nchi yetu ipate uhuru,na mafanikio haya yamechangiwa na juhudi kubwa zilizofanywa na vyombo vya ulinzi na usalama na ushiriki wa wananchi katika kutoa taarifa”inaeleza taarifa hiyo
Akizungumza na Bajeti Communication mkoani Dar es Salaam juu ya madhara ya dawa za kulevya ikiwemo kuharibika sura,kutoka meno na wakati mwingine kusimama upande bila kuanguka,Mkuu wa Kitengo cha Medhadone kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Mwananyamala mkoani Dar es salaam Dkt.Sosteus Hongo anasema waraibu wanaotembelea klini zao ni wale walioathirikana na matumizi ya heroin pekee na sio dawa zingine za kulevya.
Anasema namba kubwa ya waraibu wa dawa za kulevya ni watumiaji wa heroin pekee.
‘’Anapotumia dawa hizo za kulevya huwa inamnyika hamu ya kula na hula vyakula vitamu vitamu sana ambavyo humfanya mwili wake kukosa virutubisho vilivyomo kwenye chakula.
‘’Heroin yenyewe inaozesha meno na kwa sababu anakula vitu vitamu sana anahabaribu meno na anakosa nuru hivyo hupelekea meno kutoka yenyewe.
‘’Pamoja na meno kutoka yenyewe,wengine hutoka meno kutokana na kupigwa kwa kujihusisha na vitendo vua kihalifu kama wizi”anaeleza Dkt.Hongo
Dkt.Hongo ambaye pia ni Daktari wa Afya ya Akili na Utengemao(Mental Health and Reabilitation) anasema watumiaji wa dawa za kulevya huonekana wakiwa wamesinzia wakiwa wamesimama bila kuanguka hutokana na kutumia dawa za methadone na kutumia vilevi.
‘’Akitumia dawa na kuchanganya na pombe husababisha mfumo wake wa fahamu kuwa chini na kubaki hapo kwa muda na pindi mfumo wake ukirudi basi anashtuka’’anasema Dkt.Hongo
Dkt.Hongo anabainisha kuwa mraibu wa dawa za kulevya akitumia medhadoni anaanza kurudi kwenye hali yake ya kawaida.
‘’Kwa yule ambaye ametumia dawa za kulevya sio kwa muda mrefu sana anapokunywa dawa za medhadone anapona”anafafanuwa Dkt.Hongo
Akizungumzia kuhusu waraibu wapya wanajitokeza mbali na wale wa zamani,anasema kwa sasa idadi ya waraibu hao imepungua sana kutokana na udhibiti wake.
‘’Tunachokiona sisi uibuaji wa waraibu wapya wa heroin umepungua sana ,zamani tulikuwa tunapokea waraibu wapya 60 hadi 70 lakini sasa hivi tunapokea 20 na maeneo mengine hadi saba
‘’Hiyo imechangiwa pia na utoaji wa elimu kuhusu dawa za kulevya ikiwemo shuleni,elimu imekuwa kubwa sana na imesaidia watu kuelewa madhara ya dawa za kulevya”anaongeza Dkt.Hongo
Dkt Hongo anabainisha kuwa wafanyabiashara wa dawa hizo nchini wengi wanakamatwa sana hivyo imesaidia wauzaji wengi kuogopa.
‘’Wauzaji wengi wa dawa za kulevya wanajua kuwa ukija na ‘unga’ Tanzania hautoki’’anasema Dkt.Hongo
Hata hivyo Dkt.Hongo anaipongeza Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) kwa kazi kubwa wanayoifanya ikiwemo ujenzi wa vituo vya kutolea tiba nchini
‘’Kwa kweli Serikali ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan imefanya kazi kubwa, imeanzisha pia Kanda nyingi mpya katika maeneo mbalimbali nchini”anaongeza Dkt.Hongo

Kwa upande wake Msemaji wa Sekta ya Afya wa chama cha ACT Wazalendo Dkt Elizabeth Sanga,anasema utumiaji wa dawa ya kulevya ni njia ya watu kujitoa kwenye ‘stress’ za maisha.
Anasema kuongezeka kwa utumiaji wa pombe na vilevi vingine kama dawa za kulevya ni moja ya vielelezo vya jamii iliyokosa matumaini, na kukosa njia sahihi za kujitoa kwenye msongo wa mawazo unaosababishwa na ugumu wa maisha, mahusiano na masuala mengine ya kijamii.
‘’Hivi karibuni, pamekuwa na ongezeko la hali ya ugumu wa maisha unaoathiri wanawake na wanaume na kutokana na mila na desturi za kitanzania, wanawake wanajikuta wanatumbukia kwa urahisi kwenye aina ya uraibu ambayo wanaweza kufanya kwa siri, mfano matumizi ya dawa za kulevya kuliko kwenye ulevi kama pombe ambao mara nyingi sio siri na mwanamke kulewa kwenye jamii inachukuliwa tofauti na mwanaume.
‘’Pia, wanawake wengi wanaepuka kujihusisha na ulevi wa pombe sababu unafungamanishwa na matatizo kama unyanyasi wa kingono, ukatili wa kijinsia na mimba zisizo pangwa”anasema Dkt.Sanga
Dkt.Sanga anafafanuwa kuwa Wanawake wana hormoni iitwayo estrogen inayowafanya wapate athari itokayo ya kutumia dawa za kulevya kama cocaine na amphetamine kwa kutumia kiasi kidogo cha dawa kuliko wanaume,
Anaongeza kuwa hali hiyo ya kuwa kwenye athari ya dawa za kulevya huendelea kwa muda mrefu zaidi kuliko wanaume.
Akizungumzia matatizo ya afya ya akili yatokanayo na matumizi ya dawa za kulevya,Dkt.Sanga anabainisha kuwa ugonjwa wa Sonona (Depression) kwa kiasi kikubwa huwakumba wanawake wengi kulinganisha na wanaume.
‘’Depression ni moja ya sababu kuu ya waathirika kuingia kwenye uraibu na aina mbalimbali ya vilevi, na wanawake wengi wanaingia kwa urahisi kwenye matumizi ya dawa za kulevya kutokana na usiri wa matumizi hayo’’anaongeza Dkt.Sanga
Naye Mwenyekiti wa Umoja wa Madereva wa Pikipiki (Bodaboda) Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani Athuman Said anasema dawa za kulevya ni hatari na watu wanakuwa ‘mateja’ na kushindwa kufanya kazi za kuwaingizia kipato
Anasema wapo waliokuwa na hali hiyo ya kutumia dawa za kulevya katika eneo lao lakini walikuwa wakitokea eneo la Gongolamboto wilayani Ilala jijini Dar es Salaam.
‘’Tunachojua kuhusu dawa za kulevya ni hatari na watu wanakuwa ‘mateja’ na hawafanyi kazi, mimi katika eneo hili la bomani tupo wanachama 100 ninaowangoza lakini hatujawahi kupata elimu kuhusu dawa za kulevya zaidi ya kuona na kusikia katika vyombo vya habari
‘’Kwa hapa kwetu baadhi ya madereva wanatumia dawa za kulevya aina ya bangi hilo sikatai, lakini tunawaomba wahusika wa elimu ya dawa za kulevya kufika kwetu Kisarawe ili waweze kutupatia elimu hiyo
‘’Hii itasaidia kwa kuwa wengine husafirisha mizigo ya abiria bila kujua lakini wakipata elimu hiyo itawasaidia sana kugundua na kuongeza nguvu ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya’’anasema Saidi




Discussion about this post