NA MWANDISHI WETU,MARA
MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) kwa kushirikiana na Vyombo vya Ulinzi pamoja na wananchi imefanya operesheni kubwa ya kihistoria wilayani Tarime na Serengeti,Mkoa wa Mara kukabiliana na tatizo la uzalishaji na usambazaji wa dawa za kulevya, hususani bangi.
Operesheni hiyo iliyoshirikisha Jeshi la Polisi na Jeshi la Akiba(Mgambo) imefanyika kwa muda wa wiki tatu katika wilaya hizo kwenye vijiji vya Matongo, Nyarwana, na Weigita vilivyopo Bonde la Masinki.
Mbali na vijiji hivyo lakini pia imehusisha pia vijiji vya Nkerege, Kembwe, Nyakunguru na Iseresere pamoja na eneo la Bonde la Mto Mara.
Akizungumza mara baada ya operesheni hiyo Oktoba 8, 2024 Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA)Aretas Lyimo amesema, jumla ya ekari 3,007.5 za mashamba ya bangi zimeteketezwa katika operesheni hiyo.
Aidha amefafanuwa kuwa kilogramu 7,832.5 za bangi kavu, na kilogramu 452 za mbegu za bangi zimekamatwa, ambapo watuhumiwa 17 pia wamekamatwa na tayari wamefikishwa mahakamani.
Kamishna JeneraliLyimo amesema operesheni hii ni sehemu ya jitihada za serikali kulinda jamii dhidi ya madhara ya dawa za kulevya na amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kutoka kwa wananchi katika kutoa taarifa kuhusu shughuli zinazohusiana na dawa hizo.
Kamishna Jenerali Lyimo amefafanuwa kuwa Mamlaka imebaini kilimo cha bangi mkoani Mara kinafadhiliwa na raia wa nchi jirani ambao huwapa mitaji wakulima wa Tarime kisha bangi ikishakomaa huvunwa na kusafirishwa kwenda kuuzwa.
“Tunatoa miezi mitatu kwa wananchi wa Mkoa wa Mara kuhakikisha wanaacha kabisa kujihusisha na kilimo cha bangi.
‘’Baada ya muda huo, tutafanya operesheni kubwa kwa namna nyingine na kuhakikisha maeneo haya yanabadilishiwa matumizi na hayatumiki tena kwa kilimo cha bangi.
‘’Pia wote wanaotetea uhalifu huu watachukuliwa hatua ili kuhakikisha wananchi wote wanatii sheria za nchi”amebainisha Kamishna Jenerali Lyimo

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Tarime Meja Edward Gowele amekiri wilaya yake kukabiliwa na changamoto ya kilimo cha bangi hususani katika eneo la Bonde la Mto Mara na tayari serikali imeanza kuchukua hatua madhubuti kukabiliana na changamoto hiyo.
“Tumeanza kutoa elimu kwa wananchi kuhusu madhara ya bangi na hasara wanayoweza kuipata kwa kujihusisha na kilimo cha bangi na walio wengi wametuahidi kuachana na kilimo cha bangi”amebainisha Meja Gowele
Kwa upande wake Afisa wa Maji kutoka Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Victoria Dakio la Mara Mwita Mataro amesema lengo kubwa la bodi ni kuhakikisha rasilimali za maji zinatunzwa na kuendelezwa pasipo kuruhusu uharibifu wa aina yoyote.
“Tumejionea hali halisi ya bonde na tumeshuhudia zao la bangi likiwa limelimwa katika Bonde la mto Mara”amesema Mataro
Mataro amefafanuwa kuwa sheria za rasilimali za maji haziruhusu kilimo haramu cha zao la bangi hata mazao mengine halali yanapaswa kulimwa umbali wa mita 60 kutoka mtoni.
‘’Hao wanaolima bangi ni sehemu ya watu wanaoharibu vyanzo vya maji kwa sababu mwisho wa siku huu udongo wote mvua zitakaponyesha tope lote linatiririkka kwenda kwenye mto’’ ameongeza Mataro.
Mataro ambaye pia ni msimamizi wa Rasilimali za Maji katika Mkoa wa Mara amesema Bodi hiyo imeandaa mpango kwa kidakio cha Kaskazini ambao unataja shughuli gani zinatakiwa kufanyika kwenye vyanzo vya maji ambazo ni rafiki, na wao kama bodi watasimamia kuhakikisha mipango hiyo inatekelezwa na hifadhi ya maji inalindwa.

Naye Afisa Kilimo kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara Lepapa Molel amebainisha kuwa wakulima wengi wanalima bangi kwa kutegemea maji yanayotoka Mto Mara
“Nashauri wakulima wageuke na kuanza kulima mazao ya chakula yanayoweza kuwapa chakula na fedha kuliko bangi”ameeleza Molel




Discussion about this post