NA MWANDISHI WETU ,MARA
WANAKIJIJI wa Kijiji cha Nkerege Kata ya Kiore wilayani Tarime Mkoa wa Mara wameamua kushirikiana na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) katika zoezi la kufyeka na kuteketeza mashamba ya bangi na kuahidi kutolima tena zao hilo.
Uamuzi huo umekuja kutokana na hofu iliyojitokeza hivi karibuni kwa wananchi hao wakati wa operesheni ya kuondoa bangi, ambapo baadhi ya watu walikimbia makazi yao wakihofia kukamatwa, jambo lililoathiri shughuli zao za kijamii na kiuchumi.
Akizungumzia sakata hilo,Diwani wa Kata ya Kiore Rhobi John ameeleza kuwa wananchi wa Nkerege kwa kauli moja wameikataa bangi na kilimo hicho hakitalimwa tena kijijini hapo.
“Jana usiku wakina baba, wakina mama na vijana wote wameamua kuwa bangi haitaonekana tena, yaani sisi wenyewe tutakuwa walinzi sisi kwa sisi.
‘’Unapoona mwenzako analima ni lazima kufuatilia na kutoa taarifa lakini naishukuru ‘Cabinet’ ya wanasheria kutoka Mamlaka kwa kutoa elimu, akina mama na vijana walikuwa hawajapata elimu na walidhani hili ni zao bora kwao”amesema John
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mila katika Ukoo wa Wasweta Mzee Julius Matiku amesema,wamekubaliana kuteketeza bangi ili kuondoa tatizo hilo la kukimbiakimbia.
‘’Kijana atakayekamatwa akilima bangi, nitalipiza faini ya ng’ombe watano na kama Mzee wa Mila nina jukumu la kuhakikisha kuwa sheria zinaheshimiwa katika kijiji’’ameeleza Mzee Matiku

Naye Katibu wa mila Ukoo wa Wasweta Burima Nyawise amebainisha kuwa kama wazee, wa eneo hilo wameamua kuteketeza bangi ili waweze kulima mazao mengine kama mahindi, ufuta na kuendelea kufuga mifugo yao katika pori hilo.
“Pori hili ni safi kwa kulima kitu chochote kama vile mahindi maharage ufuta,mazao yote yanakubali,hili zao la bangi limetuchosha.
‘’Sasa watoto watulie nyumbani, wanawake wawapikie watoto, sisi malengo yetu ya kuja humu shambani ni kuhakikisha tumeliteketeza hili zao la bangi” ameongeza Nyawise.
Mamlaka ya Kudhiitia Kupambana na Dawa za Kulevya inaendelea kufanya operesheni nchi nzima ili kuhakikisha dawa za kulevya za mashambani na viwandani zinatokomezwa na Tanzania inakuwa huru dhidi ya dawa za kulevya.
Hata hivyo ni jukumu la kila mmoja kupiga vita dawa za kulevya na wananchi wasikubali kuwa sehemu ya kuangamiza taifa kwa kuendelea kulima na kufanya biashara ya dawa za kulevya




Discussion about this post