NA MWANDISHI WETU
SERIKALI ya Tanzania imeihakikishia Serikali ya Uingereza kuendeleza ushirikiano kwenye Sekta ya Madini hususani katika kujengea uwezo watu wake, kubadilishana uzoefu na uongezaji thamani madini
Mbali na hilo lakini pia kuwekeza kwenye kufanya tafiti mbalimbali ili kukuza sekta hiyo na kupanua mnyororo wa thamani utakaoongeza ajira na kuchangia katika ukuaji wa pato la taifa.
Hayo, yameelezwa Januari 8.2025 na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde katika Ofisi ndogo za Wizara ya Madini jijini Dar es Salaam wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, Marianne Young.
Mavunde amesema Balozi Young amefika ofisini kujitambulisha kwa kuwa ana muda mfupi nchini tangu awasili na wamezungumzia ushirikiano mkubwa uliopo kati ya Tanzania na Uingereza.
Ameongeza kuwa Tanzania na Uingereza zimekubaliana katika kuwajengea uwezo watu wake na kubadilishana uzoefu hususani katika Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini nchini (GST) na British Geological Survey (BGS)ya Uingereza ili kuwajengea uwezo Watanzania kwa kuwa na ujuzi stahiki katika masuala ya uendelezaji wa Sekta ya Madini
‘’Eneo la pili tulilozungumzia kwa urefu ni katika madini,mkakati ambapo Uingereza wameonesha utayari katika kushirikiana na Tanzania katika eneo la mnyororo mzima wa uongezaji thamani madini,mkakati ambapo Tanzania imejipanga kuhakikisha inavutia uwekezaji mkubwa wa ujenzi wa viwanda vya kuongeza thamani madini hapa nchini.
‘’Sasa ni muda muafaka wa kuhakikisha madini ya kimkakati yanawanufaisha Watanzania na Taifa, na ndiyo maana tumeandaa mkakati maalum wa kutekeleza azma hiyo huku ikizingatiwa kuwa madini hayo kwa sasa yana mahitaji makubwa duniani.
‘’Tupo katika hatua za mwisho kukamilisha mkakati huu maalum wa madini na muhimu ambao pia ni sehemu ya Kampeni ya Dunia katika kupunguza hewa ya ukaa kupitia matumizi ya nishati safi,” amesema Mavunde.

Akizungumza katika Mkutano huo Balozi wa Uingereza nchini Tanzania Marriane Young amesema Uingereza inapongeza jitihada kubwa za kukuza Sekta ya Madini zinazofanywa na Serikali ya Tanzania chini ya Uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuahidi kuimarisha ushirikiano mkubwa baina ya nchi hizi hasa katika kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo kupitia Taasisi za madini nchini Uingereza na Tanzania.
Balozi Young ameunga mkono mpango wa uongezaji thamani madini nchini na kuahidi kwamba Uingereza itashirikiana na Tanzania kwa ukaribu ili malengo hayo ya timie.




Discussion about this post