NA MWANDISHI WETU
CHAMA Cha African Democratic Allience ADA-(TADEA) kimesema kinajiandaa kuzindua kampeni zake za uchaguzi katika eneo la Mbagala mkoani Dar es Salaam.
Hata hivyo baada ya uzinduzi huo,chama hicho na mgombea wake wataelekea Zanzibar ambapo watafanya mikutano Unguja na kisha kuelekea Pemba kuendelea na kampeni za kuwania kiti cha urais.
Wakati chama hicho kikitarajia uzinduzi huo,tayari baadhi ya vyama vingine vya siasa vilishazindua kampeni zao kikiwemo Chama cha Mapinduzi (CCM) ambapo kilizindua kampeni zake Agosti 29,2025 katika viwanja vya Kawe mkoani Dar es Salam.
Akizungumza na Bajeti Communication kutoka mkoani Tanga Septemba 8,2025, Katibu Mkuu wa Chama hicho Salehe Msumari amesema uzinduzi huo utafanywa Septemba 14,2025 katika viwanja vya Mbagala ambapo pia watazindua na Ilani yao ya uchaguzi watakayoinadi nchi nzima ili kuwashawishi watanzania kukichagua chama hicho na kisha kupata ridhaa ya kuongoza Serikali.
Msumari amebainisha kuwa baada ya kuzinduzi wataelekea Unguja,Pemba na Tanga na kisha kuelekea mikoa mingine ikiwemo Arusha,Singida,Mbeya,Mwanza Kigoma,Katavi ambapo ratiba hiyo inaenda sambamba na ile ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC).
“Katika uchaguzi huu sisi tumewapa kipaumbele sana wanawake na watu wenye ulemavu ili kutoa fursa kwa makundi yote kugombea nafasi mbalimbali uongozi ikiwemo udiwani na ubunge katika maeneo mbalimbali nchini ambapo fomu zote tuliwaptia bure.
“Mgombe wetu wa Urais alishakidhi vigezo vyote na gari ameshapewa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) na baada ya uzinduzi ,tutaendelea kunadi sera zetu kwa wananchi”ameongeza Msumari
Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29,2025 ni wa aina yake baada ya INEC kuwapatia wagombea wote wa nafasi ya urais magari ya kisasa aina ya Land cruiser jambo ambalo halijawahi kufanyika katika historia ya uchaguzi mkuu tangu vilipoanzishwa vyama vingi mwaka 1992.
ADA-TADEA ambacho kilianzishwa na Oscar Kambona 1991 kimebainisha kuwa vyama 18 kwa sasa vinaendelea na shughuli zao za kisiasa na kichama hivyo kuhidhirisha kuwa hali ya kisiasa iko shwari.
Awali Msumari aliishukuru Serikali kwa kusikikliza malalamiko ya wadau katika baadhi ya sheria katika Tume ambapo mengi ya mambo ya msingi yamefanyiwa kazi huku ikiwashirikisha kila kitu.
Msumari ameyataja baadhi ya mambo waliyokuwa wakiyalalamikia kama vyama vya upinzani ni pamoja na kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi jambo ambalo limetekelezwa.
“Hakuna mgombea ambaye atapita bila kupingwa sasa hivi,hilo halipo,lazima mgombea apigiwe kura za ndio au hapana na kura za ndio ziwe nyingi ndio atapita lakini akipata za hapana nyingi basi Tume itaangalia.
“Mabadiliko mengine ni mfumo wa muundo wa Tume ambapo tulilalamika sana kuhusu Wakurugenzi wa Halmashauri kusimamia uchaguzi hivyo sasa hivi Tume inawafanyakazi wao”amesema Msumari.
Msumari amebainisha kuwa mbali na hayo lakini pia INEC imewakabidhi nyaraka mbalimbali zinazohusu uchaguzi ikiwemo orodha ya wapiga kura,ratiba,sheria pamoja na kuwahakikishia kuwa kampeni zifanyika kwa amani ikiwemo ulinzi kwa wagombea nafasi ya urais na katika mikutano ya hadhara.
“Sasa hivi wakala akiwa na kitambulisho cha kupigia Kura,Uraia na Leseni vinaweza kumtambulisha hata kama hana picha ambapo pia majina yote ya mawakala wanaosimamia kituo hicho yatabandikwa nje kila mtu ataona.
“Yale tuliokuwa tunayalalamikia mengi yamerekebishwa kwa asilimia 80 lakini mengine yanafanyika kutokana na utashi wa mtu binafsi na sio Tume kama Tume”amesema Msumari



Discussion about this post