NA MWANDISHI WETU
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kinaamini kuwa misingi imara ya Utawala Bora, Demokrasia, Haki za Binadamu na Utawala wa Sheria ni muhimu katika kuhakikisha kuwa Taifa linaendelea kuwa na amani na utulivu.
Hata hivyo CCM kitaielekeza Serikali yake kuhuisha na kukamilisha mchakato wa katiba mpya.
Hayo ni kwa mujibu wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 yenye kauli mbiu ‘’Kazi na Utu, Tunasonga Mbele’’ iliyotolewa Mei 2025 na kuzinduliwa Agost 28,2025 Kawe mkoani Dar es Salaam.
“Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 ni ahadi na mkataba mama kati ya CCM na Serikali yake na wananchi katika kipindi cha miaka mitano ijayo (2025 – 2030)”imeeleza Ilani hiyo
Ilani hiyo imebainisha kuwa CCM inaahidi kuendelea kuboresha uchumi, kuimarisha ustawi wa wananchi na kuhakikisha kuwa Serikali inayoiunda inaweka na kutekeleza mikakati thabiti ya kuinua hali za maisha za wananchi na kuboresha kipato chao.
“Lengo kuu la Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 ni kukuza uchumi na kuimarisha ustawi wa wananchi aidha, Ilani hii ni nyenzo ya CCM katika kuanza kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050”imefafanuwa Ilani hiyo
Katika Ahadi na Maelekezo ya CCM (2025 – 2030) ya Ilani hiyo,CCM imefafanuwa kuwa misingi imara ya utawala bora, demokrasia, haki za binadamu na utawala wa sheria ni muhimu katika kuhakikisha Taifa linaendelea kuwa na amani na utulivu.
“Katika kipindi cha utekelezaji wa Ilani hii, Chama kitaielekeza Serikali kuendelea kuimarisha demokrasia na utawala wa sheria kwa kutekeleza yafuatayo:
“Kuimarisha misingi ya demokrasia kwa kuboresha mazingira wezeshi ya wananchi kushiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii, kiuchumi na kisiasa kwa kuzingatia maadili na sheria za nchi.
“Kuhuisha na kukamilisha mchakato wa katiba mpya”imeongeza Ilani hiyo
Aidha CCM itaimarisha matumizi ya kamera za ulinzi (CCTV) na TEHAMA katika kubaini na kuzuia uhalifu na wahalifu.
“Kuanzisha mamlaka mpya na huru ya upelelezi inayojitegemea itakayojulikana kama Ofisi ya Taifa ya Upelelezi (National Bureau of Investigation) itakayokuwa na jukumu la kupeleleza makosa yote ya jinai.
“Kuboresha mishahara na maslahi ya askari wa Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza, na uhamiaji ikiwamo kupitia upya umri wa kustaafu na mafao ya pensheni.”imebainisha Ilani hiyo
Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM na Mgombea wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan,amesema Mwaka huu Taifa letu limetengeneza Dira mpya itakayoongoza mipango ya maendeleo ya nchi yetu kwa kipindi cha miaka 25 ijayo.
“CCM inaunga mkono matarajio yote yaliyoanishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, na tunaahidi kuyatekeleza kikamilifu.
“Ilani hii imezingatia kikamilifu maudhui na vipaumbele vilivyobanishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
“Kwa kipindi cha miaka mitano ijayo (2025-2030), CCM itaisimamia Serikali ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kujenga uchumi imara, jumuishi na shindani; kulinda amani usalama na utulivu; na kuimarisha ustawi wa Watanzania kwa kuwawezesha kiuchumi na kufungua fursa zaidi za ajira na biashara.”amesema Rais Samia



Discussion about this post