OTTAWA,CANADA
CANADA inapambana kuuzima moto unaondelea kuwaka katika baadhi ya maeneo ya nchi hiyo ambao unaosababishwa na kuongezeka kwa viwango vya joto.
Katika Jimbo la British Columbia la nchi hiyo, serikali imetangaza kuwa kuna moto unaowaka katika maeneo 269 ambapo 61 tu ndio umedhibitiwa.
Moto huo unawaka zaidi katika maeneo ya kati na kusini mwa jimbo hilo karibu na mpaka na jimbo la Alberta.
Canada imekumbwa na joto kali linalofikia nyuzi joto 46.1 hali iliyosababisha migahawa, maduka na shule kufungwa katika baadhi ya maeneo.
Mbali na kufungwa kwa shule na shughuli zingine za kijamii theluji pia imeyeyuka na kusababisha kuongezeka kwa kina cha maji ya mto, hali iliyopeleka wananchi kuhamishwa.
Wimbi hilo la joto, limeathiri zaidi magharibi mwa nchi hiyo, limesababisha msimu wa joto mkali zaidi katika miaka 84 iliyopita nchini humo.
Kulingana na Huduma ya Hali ya Hewa ya Canada, joto la nyuzi 46.1 lililorekodiwa katika jimbo la British Columbia.
Rekodi ya awali ya joto la juu katika historia ya nchi hiyo ilikuwa nyuzi 45 Celsius, iliyorekodiwa katika jimbo la Saskatchewan mnamo Julai 1937.
Awali mtaalam wa hali ya hewa katika Wizara ya Mazingira ya nchi hiyo Derek Lee, ,alikielezea chombo cha habari cha CBC kuwa joto litapanda zaidi kutoka nyuzi 46.1 hadi kuweza kufikia nyuzi joto 50 za Celsius katika maeneo mengine.
Discussion about this post