ATHENS,UGIRIKI
UGIRIKI inaelekea kushindwa kuudhibiti moto wa msituni unaowaka katika maeneo mengi ya nchi hiyo unaotokana na kile kinachoelezwa kuwa ni kuongezeka kwa viwango vya joto la zaidi ya nyuzi 45 za celsius linalosababishwa na mabadiliko ya tabia nchi( hali ya hewa).
Idara ya zima moto ya nchi hiyo imesema wazima moto 330, magari 115 pamoja na helikopta sita zimetumwa katika eneo la Vilia kupambana na moto huo.
Hata hivyo serikali ya nchi hiyo imewahamisha maelfu ya watu kutoka vijiji kadhaa kaskazini mwa mji mkuu, Athens kutokana na moto unaoendelea kuwaka kwa siku ya pili leo.
Moto huo wa ajabu ulianzia katika eneo la Vilia, jana Jumatatu muda mfupi tu baada ya moto mwingine kuwaka kusini mashariki mwa mji wa Athens, katika eneo la Keratea.
Idara ya zima moto imesema matukio hayo mawili ya moto ni miongoni mwa matukio mengine ya moto wa msituni iliyozuka kote nchini humo.
Awali Waziri wa usalama wa Raia wa nchi hiyo Mihalis Chrisohoidis alikiambia kituo kimoja cha luninga, kuwa wazima moto hao walipambana usiku kucha bila kupumzika kuzima moto huo katika maeneo mengine ya nchi hiyo yanayoendelea kuteketea na moto huo.
Kamanda wa vikosi vya wazimamoto nchini humo, Brigedia Jenerali Aristotelis Papadopoulos amesema Ugiriki inapita katika kipindi cha siku kigumu cha mawimbi ya joto kali zaidi ikilinganisha na miaka mengine 30 iliyopita.
Poland imetoa wazima moto 143 , wametumwa kama sehemu ya msaada wa kigeni kutoka mataifa ya Ulaya na Mashariki ya kati kuisaidia Ugiriki kukabiliana na moto huo uliozuka nchini humo wiki mbili zilizopita
Baadhi ya nchi za Ulaya zinazopakana na bahari ya Mediterania, zikiwemo Italia, Albania na Macedonia Kaskazini pia zimekumbwa na janga hilo la moto wa msituni, na kitengo cha Umoja wa Ulaya cha kupambana na majanga kimesema kinapeleka msaada wa ndege na wataalamu wa kuzima moto.
Discussion about this post