NA GOODLUCK HONGO
WATU wenye ulemavu wa miguu wameombwa kujitokeza kwa wingi kusomea fani ya udereva baada ya Mhandisi Joseph Taifa kutengeneza kifaa maalumu kinachomwezesha mtu mwenye hali hiyo kuendesha gari.
Hata hivyo Taifa ambaye ni Mtanzania amefanikiwa kutengeneza kifaa hicho kwa msaada wa fedha kutoka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) baada ya kujiridhisha na ubunifu wake ambao utasaidia jamii katika kutatua changamoto za watu wenye ulemavu wa miguu.
Akionesha kifaa hicho mbele ya waandishi wa habari na watafiti jijini Dar es Salaam Machi 8,2023 wakati wa Mafunzo ya Uandishi wa Habari za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu kati ya waandishi wa habari na watafiti yaliyoandaliwa na COSTECH,Taifa amesema kwanza anaishukuru sana Serikali kupitia Taasisi zake kama COSTECH ambazo zimemsaidia kifedha kutengeneza kifaa hicho.
Amesema yeye aliamua kubuni kifaa hicho baada ya kumaliza Chuo na kuona changamoto zinazowakuta watu wenye ulamavu wa miguu kuendsha magari hivyo aliona ni vema kufanya utafiti na jinsi gani kundi hilo litaweza kuendesha gari kama walivyo watu wasio na ulemavu wa miguu.
“Ukishapoteza miguu basi kuendesha gari ni shida na wengi wa walemavu walishakata tamaa ya kuendesha gari lakini kifaa hiki kinafungwa bila kuharibu gari lakini pia kinaweza kutolewa pia na gari kubaki katika hali yake ya awali.
“Kimefanyiwa majaribio mengi na hata Shirika la Viwango Tanzania (TBS) imekithibitisha kuwa ni salama hivyo wote wanaohitaji kufungiwa ni lazima kwanza wafundishwe kwa kwenda shule ya udereva kama walivyo madereva wengine.
“Wakati tunaendelea kutengeneza vifaa hivi lakini pia tunaendelea na maandalizi ya shule ya udereva kwa kufuata vigezo vya serikali ili mtu anapofungiwa basi ajue jinsi ya kutumia lakini vinginevyo wanaweza kusababisha ajali nyingi barabarani kwa kuwa hawana elimu ya kutumia mfumo huo kuendesha gari”amesema Mhandisi Taifa
Taifa ameongeza kuwa hadi sasa wamefanikiwa kutengeneza vifaa 22 na kati ya hivyo wamefunga magari mawili pekee ambapo gharama za kufunga kifaa hicho ni Sh.600,000 kwa gari moja
“Hizi taasisi za Serikali zinasaidia sana kutuibua maana unaweza kuwa na ubunifu mzuri lakini huna fedha za kuendeleza hivyo mimi naishukuru Serikali kupitia COSTECH kuniwezesha hadi kutengeneza kifaa hiki na kuwa na darasa maalumu la walemavu ili waweze kuvitumia.
“Tunawaomba watu wote wenye ulamavu wa miguu watutafute kwani sasa wanaweza kuendesha gari kama watu walio na viungo vyote.
COSTECH chini ya Mkurugenzi wake Dkt. Amos Nungu imefanikiwa kuwatambua wabunifu 2647 katika kipindi cha kuanzia mwaka 2018 hadi 2022.
Katika kipindi hicho pekee kiasi cha Sh.Bilioni 4.26 zimetumika kwa wabunifu 178 kuwezeshwa ili waweze kuendeleza vitu walivyobuni kwa manufaa ya kuwanufaisha wananchi.
Hata hivyo baadhi ya wananchi wameonesha kufurahishwa na kitendo cha Serikali kuwasaidia wabunifu wa Sayansi na Teknolojia kwa kuwa itasaidia zaidi nchi kuwa na wanasayansi wake hivyo kuongeza maendeleo kwa Taifa kama ilivyo kwa nchi kama China ambayo kwa sasa iko juu katika uga wa Sayansi na Teknolojia baada ya kuwaendeleza wabunifu wake.




Discussion about this post