NA MWANDISHI WETU,DODOMA
SERIKALI imesema inaendelea na jitihada za kuzitafutia ufumbuzi hoja nne za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar zilizobaki ili kuhakikisha kuwa unaendelea kudumu na kuimarika,
Hayo yameelezwa Mei 24,2023 bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Geofrey Pinda kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu Latifa Khamis Juwakali.
Pinda amezitaja hoja hizo zilizobaki kuwa ni pamoja na Mapendekezo ya Tume ya Pamoja ya Fedha, Usajili wa Vyombo vya Moto na Uingizaji wa sukari inayozalishwa Zanzibar katika Soko la Tanzania Bara.
Hoja nyingine ni Mgawanyo wa mapato yatokanayo na hisa za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) zilizokuwa katika Bodi ya Sarafu ya Afrika Mashariki na faida ya Benki Kuu.
“Hoja hizo nne zilizosalia zipo katika hatua mbalimbali za majadiliano na ni matumaini ya Serikali zetu mbili kuwa changamoto zote zitapatiwa ufumbuzi na hivyo sote tutafaida matunda ya Muungano,” amesema Pinda.
Ameongeza kuwa kwa msingi huo wizara zinazohusiana na masuala ya Muungano hukutana kwa ajili ya kujadili changamoto zinazokabili sekta zao na kuzitafutia ufumbuzi.
Desemba 6,2022 jumla ya hoja nne zilipatiwa ufumbuzi katika kikao cha Kamati ya Pamoja ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kilichofanyika jijini Dodoma.
Hoja zilizopatiwa ufumbuzi katika kikao hicho ni pamoja na Malalamiko ya Wafanyabiashara wa Tanzania Zanzibar kutozwa kodi mara mbili wanapoagiza mizigo kutoka nje ya nchi na kupeleka Tanzania Bara, Kodi ya Mapato na Kodi ya Zuio,Ongezeko la Gharama za Umeme kutoka Shirika la Umeme nchini (TANESCO) kwenda Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) pamoja na Hoja ya Mkataba wa Mkopo wa Fedha za Mradi wa Ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume (Terminal III).




Discussion about this post