NA MWANDISHI WETU,DODOMA
SERIKALI kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais imeanza kampeni ya kupanda miti mashuleni ijulikanayo kama “SOMA NA MTI” ili kuhamasisha utunzaji na uhifadhi wa mazingira.
Aidha upandaji miti na uhifadhi wa misitu ni moja ya hatua muhimu katika kukabiliana na changamoto za athari za mabadiliko ya tabianchi, hivyo kwa kutambua umuhimu huo Serikali imeamua kuanzisha “SOMA NA MTI“
Hayo yameelezwa Mei 26, 2023 na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Khamis Hamza Khamis wakati wa hafla ya zoezi la upandaji miti katika Shule ya Sekondari Buigiri iliyopo Kata ya Buigiri Wilaya ya Chamwino jijini Dodoma, na kuongeza kuwa suala la uhifadhi wa mazingira ni jambo mtambuka linalohitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali.
Amesema lengo la kampeni hiyo ni kuwafanya wanafunzi waone zoezi la upandaji miti kuwa ni sehemu ya maisha yao ili kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi ikiwemo ukame na uhaba wa maji.
Ameongeza kuwa Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa unaotolewa na sekta binafsi nchini katika kuhakikisha utekelezaji wa mipango mbalimbali ya uhifadhi wa mazingira inakuwa na mafanikio ikiwemo kuwawezesha vijana kupata elimu sahihi ya utunzaji wa miti na kuchangia uhifadhi wa mazingira kwa weledi.
“Mabadiliko ya tabianchi ni ongezeko la muda mrefu la joto la wastani la dunia na kusababisha kubadilika kwa mfumo mzima wa hali ya hewa, ili kuinusuru jamii yetu kutoka kwenye changamoto hizi tunapaswa kupanda miti kwa wingi ili kuokoa maisha ya viumbe hai wengine pamoja na binadamu” amesema Khamis.
Hata hivyo Khamis amevitaka vyombo vya habari, taasisi na wadau wa mazingira kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa utunzaji na uhifadhi wa mazingira ili kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Amebainisha kuwa viongozi wakuu wa dunia kila wakutanapo katika vikao na mikutano mbalimbali hujadili kwa kina masuala muhimu ya kidunia ikiwemo ajenda ya uhifadhi na utunzaji wa mazingira ambapo umuhimu wake unabeba mustakabali wa viumbe hai, rasilimali na maliasili zilizopo katika uso wa dunia.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Shirika la Tabora Carbon Credit Harvest (TCCHP) Bernard Mwanawille amesema Shirika hilo litaendelea kuunga mkono juhudi za serikali katika utunzaji na uhifadhi wa mazingira ikiwemo uhamasishaji wa jamii katika zoezi upandaji wa miti.
“Pamoja na kuhamasisha jamii uhifadhi na utunzaji wa mazingira, mwaka 2019 Shirika letu limeingia mkataba na Serikali katika uzalishaji wa biashara ya kaboni katika Mkoa wa Tabora ambayo tayari tumepatiwa misitu ya serikali ya mkoa na Wilaya” amesema Mwanawille.
Naye Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Riziki Lulida amesema ajenda ya Dodoma ya kijani na Tanzania ya kijani inawezekana iwapo kutakuwepo ushirikiano wa pamoja baina ya serikali, jamii na wadau katika suala la uhamasishaji wa uhifadhi na utunzaji wa mazingira.




Discussion about this post