NA GOODLUCK HONGO
KAMISHNA Jenerali wa Mamlaka ya Kuthibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Tanzania (DCEA) Aretas Lyimo amesema Mamlaka yake ipo katika hatua za kuvunja mitandao yote mikubwa ya dawa za kulevya.
Amesema DCEA itaendelea kuwakamata wafadhili na wafanyabiashara wote wa dawa za kulevya nchini na nje ya nchi ili kulinda afya za watanzania ikiwemo amani na umoja.
Kauli ya Kamishna Jenerali Lyimo imekuja wakati ambapo Mamlaka hiyo ikiwa imepata mafanikio makubwa katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya hali iliyosaidia kupungua kwa idadi ya waraibu wa dawa hizo kulikothibitishwa na mmoja wa madaktari wanaoshughulika na kuwahudumia waraibu hao.
Hata hivyo kukamatwa kwa Richard Henry Mwanri anayetuhumiwa kuwa wakala nchini Tanzania wa kupokea dawa za kulevya kutoka nchi mbalimbali duniani na kuziingiza nchini kisha kusambazwa kwa wauzaji wengine kutasaidia kuvunja mitandao hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Septemba 10,2024 Kamishna Jenerali Lyimo amebainisha kuwa wataendela kufanya operesheni mashambani,barabarani na sehemu nyingine na kuwakamata wahusika ili kulinda afya za watanzania.
Amesema mbali na hilo lakini pia wanashirikiana na nchi zinakotoka dawa hizo baada ya kupewa taarifa na watuhumiwa waliowakamata hivyo kuisaidia katika uchunguzi wao.
Kwa mujibu wa uchunguzi wa Bajeti Communication Kauli ya Kamishna Jenerali Lyimo ya kuvunja mitandao yote mikubwa ya wafanyabiashara ya dawa za kulevya inathibitishwa na Taarifa ya Hali ya Dawa za Kulevya ya Mwaka 2023 iliyotolewa Mei 2024 na kusainiwa na aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu,(Sera,Bunge na Uratibu) Jenista Mhagama kuwa ni watanzania 26 pekee ndio waliokamatwa nje ya nchi kwa kujihusisha na dawa za kulevya mwaka 2023.
‘’Mwaka 2023,watanzania 26 walikamatwa nje ya nchi kwa tuhuma za kujihusisha na usafirishaji wa dawa za kulevya.
‘’Kwa mwaka 2022 Watanzania waliokamatwa nje ya nchi kwa kujihusisha na dawa za kulevya walikuwa 147,wanaume 136 na wanawake 11’’imefafanuwa taarifa hiyo

Kutokana na kushuka kwa idadi hiyo ni wazi kuwa DCEA imefanya kazi kubwa na inapaswa kupongezwa kutokana na nguvu kubwa walizonazo wafanyabishara hao ikiwemo fedha,teknolojia,makundi ya uhalifu,mitandao ya kijamii,kumiliki njia za usafiri ikiwemo ndege na kuwepo kwa vipenyo vingi vya bandari bubu zilizopo pembezoni mwa bahari.
Hata hivyo Bajeti Communication iliwasiliana na Mkuu wa Kitengo cha Methadone kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala mkoani Dar es Salaam Dk.Sosteus Hongo ambaye ameeleza kuwa kwa sasa uibuaji wa waraibu wapya wanaotumia dawa za kulevya umepungua sana tofauti na miaka ya nyuma.
Amesema zamani walikuwa wanapata waraibu wapya hadi 60 lakini sasa hivi wanafika 20 na sehemu zingine hadi saba hivyo ni juhudi kubwa zilizofanya na Serikali hasa hii ya Awamu wa Sita inayoongozwa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan.
Dk.Hongo ambaye pia Daktari wa Afya ya Akili na Utengamao (Mental Health and Reabilitation)ameongeza kuwa udhibiti na utoaji wa elimu vimesadia sana watu kuelewa madhara ya kutumia dawa za kulevya ikiwemo utoaji wa elimu katika shule.
‘’Niseme Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imefanya kazi kubwa sana.
‘’Watu wengi wanakamatwa sana hivyo wauzaji wengi wanaogopoa lakini pia Serikali imeanzisha Kanda nyingi mpya katika maeneo mbalimbali nchini hivyo Serikali imefanya kazi kubwa sana’’amesema Dk.Hongo
Tani 1965.34 za dawa za kulevya ikiwemo heroin, zilikamatwa katika kipindi cha mwaka wa 2023 peke yake.
Kiwango hicho kinatajwa kuwa ni mara tano kwa miaka tisa iliyopita ambapo bangi imeongoza ikifuatiwa na heroin,mirungi na dawa mpya aina ya methamphetamine zikifikisha uzito kuanzia tani moja na kuendelea.
Biashara ya dawa za kulevya ni miongoni mwa uhalifu wa kupangwa unaovuka mipaka.

Hata hivyo kazi ya kupambana na kudhibiti biashara ya dawa za kulevya ndio kwanza kama inaanza kutokana na baadhi ya Serikali duniani kuandamwa na makundi ya waasi wanaodhibiti maeneo makubwa ya nchi.
Polisi nchini Guinea-Bissau siku ya jumatatu ilikamata tani 2.6 za dawa za kulevya aina ya Cocain kutoka kwenye ndege iliyowasili katika Mji Mkuu wa nchi hiyo Bissau ikitokea nchini Venezuela.
Taarifa ya Polisi ilieleza kuwa baada ya operesheni ambayo ilifanyika siku ya Jumamosi mchana kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Osvaldo Vieira wa Bissau walifanikiwa kukamata marobota 78 ya dawa za kulevya ambazo ziliingizwa kinyemela kwenye ndege ya Gulfstream IV.
Wafanyakazi watano wa ndege hiyo akiwemo rubani,ambao ni raia wawili wa Mexico,raia mmoja wa Colombia ,Ecuador na Brazil walimakatwa.




Discussion about this post