NA MWANDISHI WETU
TAASISI ya Hizb ut Tahrir Tanzania imesema kuachiwa huru kwa masheikh wa Uamsho uwe mwanzo wa kutendewa haki kwa mahabusu wengine waliobakia gerezani.
Kauli ya taasisi hiyo ya kidini imekuja siku chache baada ya Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP)Sylvester Mwakitalu kuwafutia mashitaka yaliyokuwa yanawakabili masheikh wa Uamsho ikiwemo ya ugaidi.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Mwakilishi kwa Vyombo vya Habari kutoka Hizb ut Tahrir Tanzania Masoud Msellem amesema uhuru wa Uamsho uwe mwanzo wa kutendewa haki mahabusu wengi waliobakia kwa kuwa baadhi ya sheria zinatumika vibaya.
Amesema kufutwa mashtaka ya Uamsho ni hatua muhimu ya kutia moyo, lakini huo uwe mwanzo tu wa safari ndefu kwa taasisi za kusimamia haki kwa kwenda mbali zaidi, kwa kuwa kuna mahabusu wengi wa mashtaka kama hayo ya ugaidi.
Amesema kwa mfano ndani ya Dar es Salaam pekee kabla ya kuachiwa Uamsho kulikuwa na mahabusu wa aina hiyo wengi pamoja na Arusha na Tanga.
“Ndani ya Mtwara kuna wenzetu watatu wa Hizb ut Tahrir Tanzania, Ustadh Ramadhani Moshi Kakoso , Omar Salum Bumbona Waziri Mkaliaganda ambao nao wamekuwa mahabusu kwa mashtaka kama hayo ya ‘ugaidi’kwa karibu miaka minne sasa”amesema Msellem.
Msellem amebainisha kuwa baada ya Uamsho kukaa mahabusu kwa miaka saba kwa tuhuma za ugaidi, hatima ya mashtaka hayo imewapa sura ya kuwepo utamaduni wa dhulma na uonevu ikiwemo kesi za kubambikiza kwa wasio na hatia kupitia mgongo wa sheria ya ugaidi, kama ambavyo pia inavyolalamikiwa sheria ya uhujumu uchumi.
Aidha amefafanua kuwa wao kama Hizb ut Tahrir Tanzania wanaendelea kusisitiza msimamo wao juu ya taasisi zinazosimamia haki kutekeleza majukumu yao kwa kusimamia haki.
“Mahabusu wote katika mikoa mbalimbali waachiwe huru, wapewe dhamana au kesi zao zisikilizwe kwa haraka na katika hilo tunavitaka vyombo vyote vya kusimamia haki vijizatiti katika majukumu yao hayo kwa weledi, uaminifu na haki kama alivyosema Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) Sylvester Mwakitalu ka”amesema Msellem
MWISHO

Discussion about this post