MAJENGO pamoja na shughuli za ujenzi huchangia asilimia 39 ya hewa chafuzi ya ukaa duniani.
Hiyo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkuu wa kitengo cha miji kwenye Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira duniani (UNEP) Marino Otto.
Akizungumza katika mahojiano maalum na Idhaa ya Umoja wa Mataifa, Otto amesema kiwango hicho kinajumuisha hewa chafuzi zitokazo kwenye majengo mathalani kupitia hewa itolewa nje na viyoyozi pamoja na malighafi zitumikazo kujenga majengo hayo.
Amesema majengo yaliyojengwa kwa saruji na vyuma huchangia asilimia 11 ya uchafuzi wa mazingira.
“Viwanda vya saruji vinatarajiwa kuzalisha hewa chafuzi ya ukaa asilimia tano ambayo itachochea kwa kiasi kikubwa katika mabadiliko ya tabianchi kama sekta moja. Sekta hiyo kwa kugundua changamoto hiyo inajizatiti kupunguza uchafuzi, lakini hiyo bado haitoshi.”amesema Otto
Otto amesema mbadala wa ujenzi ambao unajali mazingira ni ule unaotumia mbao ambazo amesema
“Tani moja ya saruji inatoa tani moja ya hewa ya ukaa wakati ikitengenezwa, na tani moja ya mbao kupitia miti ambako inatolewa inasaidia kuondoa tani mbili za hewa ya ukaa kutoka kwa mazingira.”
Ameongeza kuwa ni muhimu kuwa na usimamizi endelevu wa misitu kwa kuhakikisha kuwa kila mti unaokatwa mwingine unapandwa ili kuzingatia ulinzi na uhifadhi wa mazingira katika nyanja tofauti.
Katika juhudi za kupambana na hali hiyo,Serikali nchini Tanzania iliamua kuanzisha Kituo cha Kitaifa cha Kufuatilia Kaboni(NCMC) kupitia Chuo cha Misitu,Wanyama Pori na Utalii katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA).
Akizungumzia umuhimu wa Kituo hicho na mabadiliko ya tabia nchi,Mkurugenzi wa NCMC Prof.Eliakim Zahabu amesema kazi kubwa ya kituo hicho ni kuratibu upimaji,uwasilishwaji na uhakiki wa takwimu za kaboni (hewa ukaa) kwa niaba ya serikali.
“Miti hutengeneza chakula chake kwa kufyonza hewa ukaa na kutoa hewa ya oksijeni na wakati huo huo kaboni inahifadhiwa kwenye miti,hivyo basi kukua kwa miti kunatokana na kiwango cha kaboni kilichohifadhiwa kwenye mti”amesema Prof.Zahabu
MWISHO
Discussion about this post