WIZARA ya Maliasili na Utalii imesema sekta ya ufugaji nyuki ina mchango mkubwa katika maendeleo ya kijamii,kiuchumi na uhifadhi wa mazingira nchini..
Mbali na hilo lakini pia sekta ya ufugaji nyuki huboresha uhifadhi wa bioanuwai ambapo kupungua na kutoweka kwa nyuki wa asali kunaweza kutumika kama kiashirio cha kuharibika kwa mazingira.
Hayo yamo katika Sera ya Taifa ya Ufugaji Nyuki iliyoandaliwa na wizara hiyo ambayo imetolewa leo mkoani Dar es Salaam katika Maonyesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (DITF) maarufu Sabasaba yenye kauli mbiu ‘ Uchumu wa Viwanda kwa Ajira na Biashara Endelevu’ ili kuwaeleza wananchi juu ya umuhimu wa ufugaji nyuki na utunzaji wa mazingira.
Sera hiyo imefafanua kuwa licha ya kutoa mchango mkubwa wa uhifadhi wa mazingira lakini pia ufugaji nyuki ni chanzo cha chakula (asali),malighafi kwa ajili ya viwanda(mishumaa ya nta,vipodozi,nguo na mafuta ya kulainishia ),madawa na mapato kwa wafugaji nyuki.
Sera hiyo imeeleza kuwa ukadiriaji wa athari kwa mazingira ni chombo kitumikacho kusaidia katika utoaji wa maamuzi ili kuhakikisha kwamba hasara na uharibifu wa mazingira unaepukwa.
“Lengo la jumla la Sera ya Taifa ya Ufugaji Nyuki ni kuongeza mchango wa sekta hii kwa maendeleo endelevu ya Tanzania, na kuboresha uhifadhi na usimamizi wa maliasili yake kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kizazi kijacho”imeeleza sera hiyo.
Sera hiyo imebainisha kuwa inakadiriwa uzalishaji wa mazao ya nyuki nchini Tanzania unaweza kufikia takribani tani 138,000 za asali na tani 9,200 za nta kwa mwaka kutokana na makundi makubwa ya nyuki yanayokadiriwa kuwa milioni 9.2.
“Ufugaji wa nyuki ambao ni stadi na sayansi ya utunzaji wa nyuki wa asali unatoa mchango mkubwa katika kuboresha bioanuai hasa nyuki wa asali ambao hujumuisha wale waumao(Apis mellifera spp) na wale wasiouma(Trigoma au Melipona spp).
“Usimamizi wa mazingira ni jukumu la kila mtu ambapo majukumu makubwa ya taasisi za serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali ni kuisaidia jamii kwa kuwapa mwamko kuhusu hali yao na kuwaunga mkono ili wawajibike”imefafanua sera hiyo
Discussion about this post