TANZANIA inakadiriwa kuwa na hifadhi zaidi ya megawati 5000 za nishati ya jotoardhi ambazo hazijaendelezwa hadi kufikia sasa na kuanza kutumika.
Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo mkoani Dar es Salaam na Kampuni ya Uendelezaji Jotoardhi Tanzania (TGDC) katika Maonyesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (DITF) maarufu Sabasaba yenye kauli mbiu ‘ Uchumu wa Viwanda kwa Ajira na Biashara Endelevu’
TGDC ambayo ni Kampuni Tanzu ya Shirika la Umeme nchini (TANESCO) chini ya Wizara ya Nishati na ilianzishwa ili kukabiliana na upungufu wa uzalishaji wa umeme wa kutosha kutokana na sababu mbalimbali ambapo serikali iliamua kuwa na vyanzo mbalimbali vya uzalishaji wa umeme vya nishati jadidifu ikiwemo jua,upepo na jotoardhi.
Taarifa hiyo ya TGDC imefafanua kuwa mpaka sasa kuna maeneo zaidi ya 52 yenye viashiria vya nishati ya jotoardhi kutokana na tafiti za awali za kisayansi.
“Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizopo katika Bonde la Ufa la Afrika Mashariki na kujaliwa kuwa na rasilimali nyingi za nishati za jotoardhi na kukadiliwa kuwa na zaidi ya megawati 5000 na hii inaashiria kuwa Tanzania ina hifadhi kubwa ya nishati jotoardhi”imesema taarifa hiyo.
Taarifa hiyo imeongeza kuwa aina hiyo ya nishati ni ya uhakika,safi(haichafui mazingira) na ni endelevu ambapo hadi 2018 TGDC imefanya tafiti katika maeneo ya Songwe,Ngozi-Mbeya,Luhoi-Pwani,Kisaki-Morogoro,Natron-Arusha,Ibadakuli-Shinyanga na Mbaya Kiejo-Mbeya.
“Nishati ya jotoardhi ni nishati inayotokana na joto linalotoka katika miamba joto ambalo ni kali na halina ukomo hivyo huchemsha maji ya mvua yanayoingia ardhini kupitia mpasuko mbalimbali katika uso wa dunia”imeongeza taarifa hiyo.
TGDC imeongeza ni lazima mvuke unaotokana na maji hayo ya moto ufikie nyuzi joto 107 hasi nyuzi joto 300 ndipo umeme unaweza kuzalishwa kwa kutumia mitambo maalum ya kufua umeme(Turbine) ambalo huzungushwa na mvuke unaotoka ardhini kwa mgangamizo mkubwa.
Hata hivyo TGDC imebainisha kuwa mbali na kuzalisha umeme lakini pia maji hayo ya moto kutoka chini ya ardhi yanaweza kutumika kupasha moto mitambo viwandani,kupasha moto nyumba,vitalu kwa ajili ya kilimo,kukausha mazao ya kilimo.
Kazi nyingine ya jotoardhi ni pamoja na kupasha moto kwenye mabwawa ya kufugia samaki na ya kuogelea,shughuli za utalii,hutumika kama tiba,kupoza na kugandisha.
Nishati hiyo ya jotoardhi ni maji ya moto yanayotoka chini ya ardhi ambapo baadhi ya maeneo hutumika kama sehemu za kitamaduni kwa wananchi kuchemshia vyakula jamii ya mizizi kama viazi,mihogo na kisha kuoga maji hayo ili kuondoa mikosi.
Discussion about this post