SERIKALI kupitia Shirika la Umeme nchini (TANESCO) inatarajia kuanza kulijaza maji Bwawa la Kufua Umeme la Julius Nyerere(JNHPP) kwa kutumia maji ya Mto Rufiji ifikapo Novemba 15,mwaka huu.
Bwawa hilo ambalo ni la nne kwa ukubwa barani Afrika linatarajia kuzalisha megawati 2115 za umeme ifikapo mwaka 2022.
Akizungumzia kuhusu ujenzi wa bwawa hilo leo katika maonesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam,Mhandisi wa TANESCO Mwanji Mhaka amesema hadi kufikia mwezi Mei,2021 mradi huo ulikamilika kwa asilimia 52 na kazi iliyobaki ni kufunga mitambo na zingine ndogondogo.
Amesema ili umeme uzalishwe kufikia megawati hizo 2115 watafunga mashine tisa ambazo kila moja itazalisha megawati 235.
“Tunatarajia kuanzia Novemba 15,2021 tutaanza kujaza maji katika bwawa hilo hadi kufikia June 2022 tutakuwa na maji ya kutosha kwa ajili ya uzalishaji”amesema Mhandisi Mhaka.
Hata hivyo Mhandisi Mhaka amebainisha kuwa si kwamba eneo hilo limechimbwa lote ili kutengeneza bwawa bali kitakachofanyika ni kuyazuia maji ya Mto Rufiji ambayo tayarudi nyuma kilomita 100 na kisha kutengeneza bwawa hilo.
Amefafanua kuwa umeme unaozalishwa na maji ndio wa bei nafuu zaidi kuliko ule unaozalishwa na mafuta na gesi kwa kuwa wanachohitaji zaidi ni maji ya kutosha.
“Mto Rufiji unapokea maji kutoka mito mitatu mikuu ambayo ni Kilombero,Ruaha na Luwegu na mingine midogo midogo na kwa hili hatutarajii upungufu wa maji kutokana na vyanzo vingi vya maji kuingia Mto Rufiji”amesema Mhandisi Mhaka
Mhandisi Mhaka amebainisha kuwa mradi huo unatakiwa kukamilika ndani ya miezi 42 ambayo kati ya hiyo,miezi 36 ndio ilikuwa ya kujenga ambapo Juni 15,2020 ujenzi wake ulianza rasmi na utamalizika ifikapo Juni 15,2022.
“Mradi huu unajengwa na Kampuni ya Arab Contractors kwa kushirikiana na Elsewelde kutoka nchini Misri ambapo shughuli rasmi juu ya bwawa hilo zilianza mwaka 2018”amesema Mhandisi Mhaka.
Discussion about this post