MAMLAKA ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) imesema hadi kufikia mwezi Januari mwaka huu uzalishaji wa gesi asilia nchini ulikuwa futi za ujazo Bilioni 5.4 .
Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mamlaka hiyo leo mkoani Dar es Salaam katika Maonyesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (DITF) maarufu Sabasaba yenye kauli mbiu ‘ Uchumu wa Viwanda kwa Ajira na Biashara Endelevu’
PURA imesema uzalishaji wa gesi asilia katika visima vya Mnazi Bay kwa mwezi Januari 2021 ulikuwa wastani wa futi za ujazo Bilioni 2.39 kwa mwezi sawa na wastani wa futi za ujazo Milioni 74 kwa siku.
Taarifa hiyo imefafanua kuwa kwa upande wa uzalishaji wa gesi asilia katika visima vya Songo Songo ulikuwa wastani wa futi za ujazo Bilioni 3.038 kwa mwezi ambapo ni sawa na futi za ujazo Milioni 98 kwa siku.
“Hadi kufikia mwezi Januari 2021,jumla ya uzalishaji wa gesi asilia umefikia wastani wa futi za ujazo Bilioni 5.428 kwa mwezi sawa na wastani wa futi za ujazo Milioni 172 kwa siku”ilifafanua taarifa hiyo
PURA ambayo iko chini ya Wizara ya Nishati imeundwa kupitia kifungu namba 11 cha Sheria ya Petroli ya mwaka 2015, imeanzishwa kufuatia ongezeko la ugunduzi wa gesi asilia nchini na kubadilishwa kwa sheria ya Petroli.
“Dhima ya PURA ni kuthibiti shughuli za mkondo wa juu wa petroli kwa uwazi,weledi na ufanisi ili kuchangia katika ustawi wa jamii na kiuchumi kwa watanzania”imeeleza taarifa hiyo.
Hata hivyo PURA ina malengo ya kuimarisha ushiriki wa wazawa na manunuzi ya bidhaa na huduma za wazawa katika tasnia ya bidhaa za petroli.
Mbali na hilo lakini pia wanamelengo ya kuimarisha uwekezaji katika mkondo wa juu wa petroli na kuhakikisha kuwa mgao wa serikali unaongezeka.
“Majukumu ya PURA ni pamoja na kuishauri serikali juu ya masuala mbalimbali yanayohusu mkondo wa juu wa petroli,kusimamia na kudhibiti shughuli za mkodo wa juu wa petroli na kusimamia shughuli zote za miradi ya kusindika gesi asilia kwa kimiminika”imeongeza taarifa hiyo.
Discussion about this post