SHIRIKA la Umeme nchini (TANESCO) limesema Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere(JNHPP) kwa kutumia maji ya Mto Rufiji umetoa ajira zaidi ya 7400 huku watanzania wakipewa kipaumbele.
Mradi huo ambao utapelekea kupatikana kwa bwawa la nne kwa ukubwa barani Afrika linatarajia kuzalisha megawati 2115 za umeme ifikapo mwaka 2022.
Akizungumza leo mkoani Dar es Salaam katika Maonyesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (DITF) maarufu Sabasaba yenye kauli mbiu ‘ Uchumu wa Viwanda kwa Ajira na Biashara Endelevu’,Mhandisi wa Shirika hilo Mwanji Mhaka amesema hadi kufikia mwezi Mei,2021 mradi huo ulikuwa na wafanyakazi zaidi ya 7400.
Amesema kati ya hao asilimia 89.09 ni watanzania na wageni ni asilimia 10.91 ambapo wanawake ni zaidi ya 270 waliopata ajira katika mradi huo.
“Kwa sasa mradi upo kwenye kilele ambapo hadi kufikia Mei 2021 ujenzi wa bwawa hilo ulifikia asilimia 52 na kazi iliyobaki sasa ni kufunga mashine na kazi nyingine ndogondogo hivyo wafanyakazi wataendelea kupungua wakati mradi unaelekea kukamilika kwa kuwa kazi nyingi zitakuwa zimekamilika ”amesema Mhandisi Mhaka
Mhaka amebainisha kuwa wafanyakazi watapungua kwa kuwa kazi nyingi zitamalizika na zilizobaki ni za kufunga mashine ambapo ifikapo Novemba 15,2021 wataanza kujaza maji katika bwawa hilo.
Akizungumzia kuhusu faida zitakazopatikana kwa upande wa vijiji vinavyozunguka bwawa hilo,Mhaka ameeleza kuwa baada ya umeme kuanza kuzalishwa vijiji hivyo vitafaidika na ujenzi wa huduma za kijamii.
“Vijiji vitajengewa Hospitali,Shule,Visima vya Maji,Vituo vya Polisi na ujenzi wa barabara na gharama za umeme zitapungua zaidi”amesema Mhaka
Akizungumzia kuhusu ujenzi wa barabara zinazoelekea katika mradi huo,Mhaka amefafanua kuwa kipande cha barabara kinachoanzia eneo Fuga hadi ndani ya mradi kitajengwa kwa lami na barabara inayopita Ubena Zomozi,Ngerengere,Mvua,Kisaki hadi eneo la mradi zitaimarishwa zaidi.
“Barabara ya Kibiti,Mloka hadi eneo la mradi nayo itajengwa ili kuhakikisha kuwa inapitika wakati wote”amesema Mhandisi Mhaka
Discussion about this post