UTURUKI imesema kuwa moto wa msituni uliowaka katika majimbo 35 ya nchi hiyo umedhibitiwa lakini vita dhidi ya kupambana na janga hilo inaendelea.
Hali hiyo inatokana na joto kuongezeka katika viwango vya juu katika baadhi ya nchi za Bara la Ulaya,America na Asia kutokana nakile kinachoelezwa na wataalamu kuwa ni mabadiliko ya tabianchi na kupelekea misitu kuwaka moto na barafu kuyeyuka kwa kasi.
Kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Habari la Nchi hiyo (TRT), Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Fahrettin Altun, alitoa taarifa hiyo akisema kuwa vita dhidi ya moto wa misitu ulioathiri nchi hiyo inaendelea kwa kuhamasisha njia zote za serikali.
“Moto 122 kati ya 129 katika majimbo 35 yamedhibitiwa.”amesema Altun
Awali Julai 31,2021 Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdoğan alifanya mazungumzo ya simu na Rais wa Urusi Vladimir Putin juu ya mambo mbalimbali ikiwemo moto.
Kulingana na taarifa iliyoandikwa na kutolewa na Ikulu ya Rais wa Urusi (Kremlin), moto wa misitu nchini Uturuki ulijadiliwa katika mazungumzo ya simu kati ya Rais Erdoğan na Rais Putin.
Rais Erdoğan alimshukuru Rais Putin kwa kutoa ndege tano za kuzima moto na helikopta tatu zaidi kusaidia vita vya Uturuki dhidi ya moto unaowaka katika misitu ya nchi hiyo unaosababishwa na ongezeko la joto.
Rais Putin alisisitiza kuwa wataendelea kuisaidia Uturuki katika kuzima moto huo.
Discussion about this post