MKAZI wa Yombo Manispaa ya Temeke mkoani Dar es Salaam,Lukuman Ally amehukumiwa kifungo cha maisha jela baada ya Mahakama ya Wilaya Temeke kumkuta na hatia kwa kosa la kumlawiti mtoto wa kiume mwenye umri wa miaka tisa.
Inadaiwa kuwa mwezi Mei mwaka 2020 maeneo ya Yombo njia panda ya Mwinyi Wilaya ya Temeke mshtakiwa huyo alimlawiti mtoto huyo huku akijua kufanya hivyo ni kosa la kisheria.
Hukumu hiyo imetolewa na Hakimu Mkazi Mwandamizi,Jimson Mwankenja ambapo amesema mahakama hiyo imejiridhisha na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka hasa mtoto aliyefanyiwa kitendo hicho.
Mwankenja amesema alipopitia ushahidi hasa wa mtoto mwenyewe mahakama hiyo imeridhika kuwa mshtakiwa alifanya tendo hilo hivyo inamtia hatiani .
“Jamhuri ilileta mashahidi watano ambao ni mama mzazi wa mtoto huyo,Daktari wa Hospitali ya Mkoa wa Temeke,Emanuel Shija,Mwalimu wa Shule,mpelelezi wa Kituo cha Polisi Chang’ombe,WP3515 Catherine ,mhanga mwenyewe na kielelezo kimoja cha PF3 huku mshtakiwa akijitetea mwenyewe “amesema Mwankenja.
Amesema mtoto huyo wakati anafanyiwa tendo hilo alikuwa darasa la tatu na alikuwa anaishi na mama yake ambapo walikuwa wamepanga nyumba moja na mshtakiwa huyo.
Mwankenja ameongeza kuwa mshtakiwa huyo alikuwa na tabia ya kupika wali na kuwaalika watoto wote wa wapangaji kula nao chakula ndani na wakishamaliza anawatoa huku akimbakisha ndani mtoto huyo peke yake na kuanza kumfanyia vitendo hivyo.
“Kwa maelezo ya mtoto amedai alimfanyia vitendo hivyo mara nne na hakuweza kumwambia mama yake kutokana alikuwa mkali hata hivyo aliyegundua Mwalimu wake alivyokuwa akitembea na anavyokaa akamuuliza na kumjibu ni uncle Lukuman amekuwa akimlawiti”amesema Mwankenja
Hakimu Mwankenja amefafanua kuwa Mahakama hiyo baada ya kuangalia kifungu cha 154(2) cha kanuni ya adhabu,uzito wa kosa,maslahi ya umma,maslahi ya mshtakiwa mwenyewe,uwepo wa kosa la ulawiti katika Wilaya hiyo na shufaa zilizowasilishwa na Wakili wa Serikali hivyo Mahakama inakupa adhabu ya kifungo cha maisha jela”amesema Mwankenja
Awali Wakili wa Serikali,Anna Chimpaya aliiomba Mahakama hiyo itoe adhabu kali kwa mshtakiwa huyo kwa kuwa vitendo hivyo vimekuwa vikiongezeka katika Wilaya hiyo.
Discussion about this post