NA MWANDISHI WETU
MKUU wa Mkoa wa Dar es salaam Amos Makalla amewataka watu wote waliojiunganishia mabomba katika bomba kuu la kusafirisha mafuta kutoka bandarini kuelekea kwa wafanyabiashara kujisalimisha mara moja.
Makalla ametoa agizo hilo leo August 20,2021 wakati akikagua kifaa cha kisasa cha kubaini wizi na upotevu wa mafuta ghafi (Radio detector) kutoka bomba kuu la kupokea mafuta kutoka kwenye meli kuelekea kwa wafanyabiashara.
Amesema kupatikana kwa kifaa hicho kitasaidia kubaini wote walio na ya wizi na kuchepusha mafuta kutoka bomba kuu ambapo kifaa hicho kinatarajiwa kuanza zoezi la ukaguzi muda wowote kuanzia sasa na kuwataka wale wote waliojiunganishia kujisalimisha.
Amesema hadi sasa tayari vyombo vya ulinzi na usalama vimewakamata na kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wa wizi huo.
Makalla amewahakikishia wafanyabiashara wa nishati hiyo kuwa serikali imejidhatiti kumaliza kabisa tatizo la upotevu wa mafuta na anashukuru kuona hadi sasa kumekuwa na matokeo mazuri.
Hata hivyo ameipongeza TPA kwa mapinduzi makubwa ya maboresho ya huduma kwa Wananchi baada ya kutembelea ujenzi wa barabara za kuingia na kutoka bandarini na upanuzi wa eneo la kushusha na kupakia mizigo.
Discussion about this post