RAIS wa Ufilipino Rodgrido Duterte mwenye umri wa miaka 76 amekubali kuwa mgombea mwenza (makamu wa rais) katika Uchaguzi wa Mkuu wa nchi hiyo unaotarajiwa kufanyika mwaka 2022.
Duterte ambaye anajulikana kwa vituo na kuwashughulikia wauzaji wa dawa za kulevya nchini humo anashutumiwa na makundi ya kutetea haki za binadamu kutokana na mauaji ya watu hao katika oparesheni za kuwasaka wahusika wa biashara hiyo.
Rais huyo ambaye kabla ya kushika wadhifa huo alikuwa meya wa jiji la Davao,amekubali idhini ya chama chake cha PDP-Laban kufuatia kile kilichoelezwa kuwa ni wito wa wengi wa kutaka uongozi dhabiti ambao utahakikisha muendelezo wa mipango ya serikali.
Makamu wa rais wa chama hicho Karlo Nograles amesema Rais Durtete amekubali kujitolea na kusikia kilio cha watu na kukubali kuidhinishwa na chama cha PDP-Laban ili kugombea kama makamu wa rais katika uchaguzi wa 2022.
Amesema chama kinapanga mkutano wa kitaifa mnamo Septemba 8 ili kuwajadili wagombea wengine katika uchaguzi wa kitaifa wa 2022.
Katiba ya Ufilipino, rais anaongoza kwa muhula mmoja tu wa miaka sita, na utawala wa Durtete utamalizika Juni 2022.
Hata hivyo wakosoaji wake wanaonya kuwa huenda anajaribu kubaki madarakani kwa kugombea kama makamu wa rais.
Septemba 2016,Dutrete alijifananisha na aliyekuwa Kiongozi wa Ujerumani Adolf Hitler baada ya kusema kuwa yuko tayari kuwamalizia maisha watumiaji wa mihadharati milioni tatu wanaopatikana katika taifa hilo.
Rais Duterte katika mazungumzo yake na waandishi wa habari aliwaeleza kuwa
“kama Hitler aliweza kuua mamilioni ya Wayahudi basi na mimi nitafurahi nikiwamalizia maisha watu milioni tatu watumiaji wa mihadharati ili kuokoa kizazi kijacho.”
Tangu rais huyo aanzishe kampeni ya kuwaua walanguzi na watumiaji wa madawa ya kulevya inadaiwa kuwa zaidi ya watu 3000 wameauwa na polisi katika kampeni hiyo
Katika moja ya vituko vya rais huyo alitishia kuwafunga jela watu watakaokataa kupata chanjo dhidi ya ugonjwa wa UVIKO-19(COVID-19) wakati taifa hilo likipambana na mlipuko mbaya zaidi barani Asia.
Discussion about this post