TANZANIA ina nguruwe wanaofikia milioni 3.2 wanaofugwa na wakulima mbalimbali nchini ambapo upande wa Zanzibar wanyama hao wamefikia 2,209.
Hayo ni kwa mujibu wa Sensa ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ya Mwaka wa Kilimo 2019/20 katika Ripoti ya Matokeo Muhimu kwa Sekta za mazao,mifugo na ufugaji wa samaki iliyotolewa Agosti mwaka huu na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS).
Katika Sensa hiyo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ya mwaka wa kilimo 2019/20 ilihusisha aina mbalimbali za mifugo inayofugwa nchini.
Aidha aina kuu za mifugo iliyoainishwa katika taarifa hiyo ni ng’ombe, mbuzi, kondoo, nguruwe na kuku.
Kwa mujibu wa Ripoti ya Matokeo Muhimu kwa Sekta za mazao,mifugo na ufugaji wa samaki, taarifa kuhusu idadi ya mifugo zilikusanywa Agosti mosi, 2020, na taarifa nyingine za mifugo zilikusanywa kwa kufuata mwaka wa kilimo wa 2019/20.
Katika ripoti hiyo maalum,matokeo hayo ya Sensa yanaonesha kuwa, idadi ya nguruwe ni 3,208,495, kwa upande wa wakulima wadogo Tanzania Bara wanyama hao walikuwa 3,201,163 na upande wa Zanzibar kwa wakulima wadogo walikuwa ni 2,209
Kwa upande wa mashamba makubwa wanyama hao walikuwa ni 5,123 kwa Tanzania Bara na upande wa Zanzibar walikuwa sifuri.
“Ujumbe muhimu wa Sensa hiyo ni kwamba idadi ya mifugo imekuwa ikiongezeka katika vipindi vitatu vya Sensa (2002/03, 2007/08 na 2019/20).
“Uhusiano wa Kisera, ongezeko la idadi ya mifugo linaweza kuwa limechangiwa na sera inayolenga kuongeza uzalishaji wa mifugo wa kibiashara ili kuweza kufikia viwango vya masoko ya ndani na nje, kuongeza kipato cha wafugaji na kuboresha hali ya maisha ya wafugaji.
“Ongezeko la idadi ya mifugo haliakisi mchango wa sekta hii kwenye Pato la Taifa ambao umeendelea kubakia chini ya asilimia mbili”ilibainisha ripoti hiyo.
Discussion about this post