KOROSHO imetajwa kuwa ndio zao kuu la biashara lililolimwa kwa kiasi kikubwa Tanzania Bara likifuatiwa na Pamba huku Zanzibar ikiongoza kwa Karafuu.
Mazao hayo ni miongoni mwa mazao makuu ya biashara yaliyozalishwa Tanzania katika mwaka wa Kilimo 2019/20 yakiwemo Kahawa na Chai,
Hayo ni kwa mujibu wa Sensa ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ya Mwaka wa Kilimo 2019/20 katika Ripoti ya Matokeo Muhimu kwa Sekta za mazao,mifugo na ufugaji wa samaki iliyotolewa Agosti mwaka huu na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS).
Ripoti hiyo ya NBS imebainisha kuwa uzalishaji wa mazao makuu ya biashara kwa Tanzania Bara ulikuwa ni tani 872,578 na Tanzania Zanzibar tani 2,447.
“Zao Kuu la Biashara lililoripotiwa kuzalishwa kwa kiasi kikubwa Tanzania Bara ni Korosho, iliyozalishwa tani 391,110, likifuatiwa na zao la Pamba tani 331,524 na Kahawa tani 82,478.
“Kwa upande wa Tanzania Zanzibar, Zao Kuu la Biashara lililozalishwa ni Karafuu, ambapo jumla ya tani 2,438 zilizalishwa”imeongeza ripoti hiyo.
Ripoti hiyo imeeleza kuwa jumla ya eneo lililopandwa mazao hayo ni hekta 1,311,035 ambapo hekta 1,291,751 zililimwa na wakulima wadogo na mashamba makubwa ni hekta 19,284
“Zao la korosho lilipandwa kwenye eneo la hekta 811,733 ambapo wakulima wadogo walipanda hekta 808,143 na mashamba makubwa yalipandwa hekta 3,590 ambalo ni eneo kubwa kwa mazao makuu ya biashara.
“Zao la pamba lilipandwa kwenye eneo la ukubwa wa hekta 314,601 ambapo wakulima wadogo walipanda hekta 313,370 na mashamba makubwa yalipandwa hekta 1,231,Kahawa ikipandwa hekta 157,999 huku wakulima wadogo wakipanda hekta 151,408 na mashamba makubwa hekta 6,591” imefafanua ripoti hiyo.
Uzalishaji wa zao la korosho uliongoza kwa tani 391,119 ambapo wakulima wadogo walizalisha tani 390,412 na mashamba makubwa tani 707), ikifuatiwa na uzalishaji wa zao la Pamba lililofikia tani 331,524 huku wakulima wadogo wakizalisha tani 330,845 na mashamba makubwa tani 679.
Kwa upande wa Kahawa ilizalishwa tani 82,478 ambapo wakulima wakubwa walizalisha tani 75,323 na wakulima wadogo tani 7,155.


Discussion about this post