NA MWANDISHI WETU
TANZANIA inakadiriwa kuwa na kuku zaidi ya milioni 83.28 ambapo kati ya hao,wa kisasa ni milioni 44.5 huku Sekta ya Mifugo ikichangia asilimia 7.4 katika Pato la Tafa.
Hayo ni kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi,Idara ya Uzalishaji na Masoko katika Mashamba ya Kuzalisha Mifugo iliyotolewa hivi karibuni.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa kuku wa asili wanafikia milioni 38.77 ambapo Sekta ya Mifugo ilikuwa kwa asilimia tano katika mwaka 2019/2020.
“Tanzania inakadiriwa kuwa na Ng’ombe milioni 33.4,Mbuzi milioni 21.29 na Kondoo milioni 5.65.
“Aidha hapa nchini kuna kuku milioni 83.28 kati ya hao,kuku wa asili ni milioni 38.77 ,na kuku wa kisasa ni milioni 44.5,Nguruwe milioni 2.14 na Punda 657,389 ”imefafanua taarifa hiyo
Aidha imeongeza kuwa Sekta ya Mifugo ilikuwa kwa asilimia tano mwaka 2019/2020 na kuchangia asilimia 7.4 ya Pato la Taifa.
Kwa upande wa Ng’ombe wa Maziwa taarifa hiyo imebainisha kuwa mwaka 2019/2020 wanyama hao walifikia milioni 1.9 ambapo mitamba ya ng’ombe wa maziwa iliyozalishwa ilifikia 18,255 na kusambazwa kwa wafugaji nchini.
“Serikali inamiliki na kuendesha mashamba matano ya kuzalisha ng’ombe bora wa maziwa na kuuza kwa wafugaji wanaohitaji ng’ombe wa maziwa.
“Aidha uzalishaji wa mitamba katika mashamba haya ni mdogo ukilinganisha na mahitaji ya wafugaji hapa nchini,hivyo kuna haja ya sekta binafsi kuwekeza katika miradi ya kuzalisha mitamba na kuuza kwa jamii ikiwa ni kuunga mkono juhudi za serikali”imefafanua taarifa hiyo
Hata hivyo lengo ni kuzalisha ndama 1,000,000 wa maziwa kwa mwaka na hivyo kuongeza idadi ya ng’ombe walioboreshwa hapa nchini.
“Mashamba ya Serikali kwa ajili ya kuzalisha mifugo ni matano,ambayo ni Sao Hill-Iringa,Kitulo-Njombe,Mabuki-Mwanza,Ngerengere-Morogoro na Nangaramo-Mtwara”imeongeza taarifa hiyo.

Discussion about this post