NA MIRIAM SARAKIKYA,ARUSHA
WAKULIMA nchini wametakiwa kutumia njia za asili katika kuzuia wanyamapori kuharibu mazao yao wakati Serikali ikichukua hatua madhubiti katika kupambana na wanyama hao.
Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru mkoani Arusha Zainabu Makwinya wakati akitoa ufafanuzi katika Kikao cha Baraza la Madiwani baada ya kuibuka kwa hoja za wanyamapori kuvamia mashamba ya wananchi zilizotolewa na baadhi ya madiwani.
Amesema Serikali inaendelea kufuatilia fedha za fidia za wakulima wa halmashauri hiyo ambao mazao yao yaliharibiwa na wanyamapori.
Makwinya amefafanua kuwa ulipwaji wa fidia kwa Wakulima 30 wa Kata ya Songoro unafuatiliwa kwani awali wananchi wengine walipatiwa fidia pasipo kufuata utaratibu wa kutoa taarifa kwa viongozi na nyingine ambazo zinapakana na maeneo ya Hifadhi ya Wanyamapori.
Makwinya ameahidi kutembelea maeneo yaliyo mpakani na hifadhi ili kuweka vizuizi vya asili ambavyo vitawazuia wanyamapori wakali kushambulia mazao ya Wakulima.
Awali baadhi ya madiwani wamesema pamoja na wakulima hao kupata hasara ya mazao yao kila mara Serikali imekua ikitoa fidia pasipo kutoa taarifa kwa viongozi wa maeneo husika hivyo fidia hiyo haiwafikii walengwa wote.
Diwani wa Kata ya Ngarinanyuki Aminieli Mungure ameiomba Serikali kufuata utaratibu wa kutoa fidia hizo ili kuhakikisha zinawafikia walengwa wote
Naye Afisa Maliasili na Utalii wa Halmashauri hiyo Charles Mungure amesema wataendelea kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kuzuia mazao yao kushambuliwa na wanyamapori
Amesema ni vizuri kwa wananchi kutowauwa wanyamapori wanaovamia mashamba yao na kutoa taarifa sehemu husika lakini kuwauwa ni kosa kwa mujibu wa sheria.
Discussion about this post