KATIKA hali isiyotarajiwa viongozi wa kijeshi waliofanya mapinduzi nchini Guinea wamewaachia huru wapinzani wote wa kisiasa wa rais aliyepinduliwa Alpha Conde.
Kuachiwa huru kwa wafungwa wa kisiasa kumekuja wakati ambapo Jeshi la nchi hiyo kupitia Kikosi Maalum lilifanya mapinduzi siku ya jumapili na kuchukua madaraka hali iliyolaaniwa na Jumuia za Kimataifa ukiwemo Umoja wa Mataifa
Hata hivyo shangwe zililipuka katika miji mbalimbali ya nchi hiyo ukiwemo Mji Mkuu Conakry kwa wananchi kushangilia kitendo hicho cha jeshi kwa kufanya maandamano wakiwa karibu na wanajeshi wanaofanya doria mitaani kuwaunga mkono.

Kwa mujibu wa Shirika la habari la Ufaransa AFP liliwashuhudia baadhi ya wafungwa wapatao 20 wakiachiwa kutoka gereza la mjini Conakry.
Mawakili wanaowatetea wafungwa hao wamesema watu 79 wamekamilisha mchakato wa kuachiwa huru kufuatia mazungumzo na viongozi wa jeshi.
Uamuzi huo umechukuliwa huku Jumuiya ya Uchumi ya Nchi za Afrika Magharibi (ECOWAS) ikijiandaa leo kujadili mzozo uliojitokeza katika nchi hiyo.
Mapinduzi ya Jumapili yamekosolewa na Marekani, Umoja wa Ulaya na ECOWAS. Urusi nayo imetaka taasisi zote za Guinea ziruhusiwe kufanya kazi haraka iwezekanavyo.
Discussion about this post