MKUU wa Mkoa wa Dar es salaam Amos Makalla amezihakikishia Kaya zote 644 za wakazi wa Magomeni Kota kuwa Serikali itawapatia makazi wote wanaostahili.
Amesema makazi hayo yatatolewa kwa wote walioainishwa tokea awali ambapo amewataka kuwapuuza wote wanaosambaza taarifa za uvumi.
Makalla amesema hayo leo mkoani Dar es Salaam wakati alipofanya ziara ya kujiridhisha na kukagua maendeleo ya mradi huo wenye thamani ya Sh.Bilioni 52.1

Mradi huo ambapo kwa sasa ujenzi wake umefikia asilimia 99 ambapo pindi utapokamilika utawanufaisha watu zaidi ya 3,000 kutoka Kaya 644 huku hatua inayoendelea sasa ni kuweka miundombinu ya umeme.
Hata hivyo Makalla amefafanua kuwa mradi utakapokamilika wakazi husika wataitwa na kutangaziwa tarehe rasmi ya kuingia katika nyumba hizo hivyo wawe watulivu.
Makalla amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutekeleza ahadi yake ya kusimamia na kukamilisha miradi yote ya maendeleo na hiyo inajirihidhisha kupitia Mradi wa Magomeni Kota.
Mradi wa Magomeni Kota ulianza October mosi, 2016 ukihusisha ujenzi wa majengo matano yenye ghorofa nane na tisa ambapo wanufaika waliokuwa wakazi wa nyumba za awali kabla ya ujenzi huo wataishi bure kwa miaka mitano.

Discussion about this post