UTAFITI uliofanywa nchini Marekani umeonesha kuwa wanawake wanaongoza kumiliki silaha za moto kuliko wanaume kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo vurugu za uchaguzi wa rais wa nchi hiyo uliofanyika mwaka 2020
Utafiti wa kitaifa kuhusu hali ya umiliki wa silaha za moto katika mwaka huu wa 2021 uliofanywa na wataalamu wa Kitivo cha Afya ya Jamii katika Chuo Kikuu cha Harvard nchini humo umeonesha kuwa, kuanzia Januari 2019 hadi Aprili mwaka huu, wanawake wapatao milioni 5.3 wa Kimarekani wamenunua silaha kwa mara ya kwanza.
Karibu wanaume milioni nne wa nchi hiyo, nao pia walinunua silaha katika kipindi hicho.
Mtafiti wa Kitivo hicho Afya ya Jamii katika Chuo Kikuu cha Harvard, Dk.Deborah Azrael amesema utafiti wao, walichunguza rekodi za watu 19,000 na kwamba huo ulikuwa utafiti mpana na jumuishi zaidi kitaifa kufanywa nchini Marekani kuhusiana na ununuzi wa silaha.
Amesema sababu ya kuongezeka idadi ya wanawake wanaonunua silaha nchini Marekani ni kutokana na ugonjwa wa UVIKO-19, malalamiko ya kijamii, yakiwemo yale yaliyogubikwa na machafuko kufuatia mauaji ya Mmarekani mweusi George Floyd yaliyofanywa na askari polisi wa jimbo la Minnesota, na machafuko ya uchaguzi wa rais wa nchi hiyo wa mwaka 2020.
Hata hivyo Utafiti huo umeonesha pia kuwa, asilimia 55 ya wanunuzi wapya wa silaha nchini humo ni wazungu, asilimia 21 ni Wamarekani weusi na asilimia 19 ni wale wenye asili ya Latini.
Kwa upande wa wanunuzi wanawake, Wamarekani weusi wanaunda asilimia 28 tu ya wanunuzi hao wa silaha za moto.


Discussion about this post