WAKATI Dunia ikikabiliana na wimbi la ugonjwa wa UVIKO-19,Japan inatarajia kupokea msaada wa mitungi 1000 ya gesi ya Oksijeni kutoka Taiwan licha ya kuwa nchi hiyo ni miongoni mwa mataifa yaliyoendelea zaidi duniani.
Mbali na kuendelea kwa nchi hiyo lakini pia imepiga hatua kubwa katika Nyanja ya Teknolojia hivyo kupokea msaada huo ni ishara ya wazi kuwa nchi hiyo imeelemewa na wagonjwa wa UVIKO-19.
Hata hivyo Taiwan itapeleka takribani vifaa 10,000 vya kupimia kiwango cha oksijeni kwenye damu, yaani pulse oximeter.
Japan inatarajiwa kupokea msaada huo katika kusaidia wagonjwa wa virusi vya UVIKO-19 wakati huu ambapo nchi hiyo ikikumbwa na uhaba wa vifaa hivyo vya kitabibu.
Mitungi ya gesi ya oksijeni inatumika na watu walioathirika wanaojitibu nyumbani na wagonjwa wanaosubiri kulazwa hospitalini.
Lakini Japani hivi sasa inakabiliwa na uhaba wa vifaa hivyo.
Kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Habari la Japan (NHK) imefafanua kuwa Wizara ya Afya ya nchi hiyo inapanga kusambaza mitungi hiyo kwenye taasisi za tiba na vituo vingine kote nchini humo kupitia serikali za maeneo.
Msaada wa Taiwan unakuja wakati wizara hiyo ikipanga kupata hadi mitungi 500 ya gesi ya oksijeni kwa mwezi kutoka kwa watengenezaji na kuikodisha mitungi hiyo katika mikoa.
Serikali ya Japani awali iliipatia Taiwan takribani dozi milioni 3.4 za chanjo ya virusi vya UVIKO-19 ya AstraZeneca


Discussion about this post