KATIBU Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres, ameelezea wasiwasi wake kwamba ulimwengu hauelekei kufikia malengo kadhaa ya dharura katika vita dhidi ya mabadiliko ya hali ya hewa.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini New York nchini Marekani,Guterres amesema kulingana na ahadi za sasa za nchi wanachama, ulimwengu uko kwenye hali mbaya ya kufikia nyuzi 2.7 Celsius za joto, badala ya nyuzi 1.5 Celsius ambayo wote walikubaliana iwe kikomo.
Kwa mujibu wa Sauti ya Amerika,Guterres amesema sayansi inawaambia kuwa kitu chochote kilicho juu ya nyuzi 1.5 kitakuwa janga,
“Ninaamini bado kuna kazi kubwa ya kufanya kuhusiana na kupunguza gesi chafu na karibu asilimia 80 ya gesi chafu ni kutoka mataifa tajiri ya kundi la G20”amesema Guterres
Umoja wa mataifa unasema, ili kufikia nyuzi 1.5 mataifa tajari yanapaswa kuwekeza dola billioni 100 kwa mwaka kati ya hivi sasa na mwaka wa 2025.
Uzalishaji wa gesi chafu pia unatakiwa kupunguzwa kwa asilimia 50 ifikapo mwaka wa 2030 kufikia lengo la kuwa na hewa safi ya carbon mwaka wa 2050.
Hii inajumuisha kazi ngumu ya kuzishinikiza nchi kuachana na viwanda vya mkaa wa mawe ambavyo vinachafua mazingira.
Mwezi Novemba, mataifa ya dunia yatakutana mjini Glasgow nchini Scotland kwenye mkutano muhimu wa kutathmini hatua iliyopigwa kwenye ahadi zilizotolewa tangu usainiwe mkataba wa Paris wa mwaka wa 2015 kuhusu hali ya hewa


Discussion about this post