SHIRIKA la Reli Tanzania (TRC) limeendelea kuboresha huduma zake za usafirishaji wa abiria na mizigo baada ya kufunga behewa zaidi ya 20 zikiwa na mbolea kuelekea mkoani Kigoma.
Mbolea hizo kutoka Kampuni ya Yara zinazofikia zaidi ya tani 800 zinasafirishwa kutoka mkoani Dar es Salaam kuelekea Kigoma katika kuhakikisha kuwa msimu wa Kilimo wakulima hawawezi kukosa bidhaa hiyo.
Akizungumzia hali ya usafirishaji wa mizigo na abiria katika Shirika hilo mkoani Dar es Salaam jana,Meneja wa TRC Kanda ya Dar es Salaam Jonas Afumwisye amesema TRC haisafirishi abiria pekee bali hata mizigo mikubwa katika hali ya usalama zaidi na kwa wakati mmoja.
Amesema ni muhimu kwa wadau mbalimbali wakiwemo wafanyabishara kulitumia shirika hilo kusafirisha mizigo yao kwa uhakika kutokana na maboresho mbalimbali yaliyofanyika na yanayoendelea kufanyika ili kutoa huduma kwa ufanisi.
“TRC inauwezo wa kubeba mzigo mkubwa kwa wakati mmoja na hapa tuna treni yenye mabehewa zaidi ya 20 yakiwa na tani zaidi ya 800 za mbolea kueleka Kigoma.
“Mzigo huu kama ungetumia barabara basi malori zaidi ya 40 yangetumika kuusafirisha lakini kwa sisi tunausafirisha kwa pamoja na kwa wakati hivyo tunawakaribisha wadau wengine kutumia TRC kusafirisha mizigo yao”amesema Afumwisye

Mabehewa ya mizigo ya Shirika la Reli Tanzania (TRC)
Baadhi ya wafanyabiashara waliozungumzia kuboreshwa kwa TRC wamesema kutumia usafiri wa treni kusafirishia mizigo kunasaidia pia utunzaji wa barabara kwa kuwa tani hizo ni nyingi na yangetumika malori mengi kusafirishia mizigo huo.
Mkurugenzi wa TRC Masanja Kadogosa amekuwa akisimamia kikamilifu shughuli za shirika hilo ili kuhakikisha kuwa linatoa huduma bora na za kisasa katika kuhakikisha kuwathamani ya fedha za walipa kodi zinatumika kama inavyokusudiwa.




Discussion about this post