ALIYEKUWA Mgombea Ubunge wa Jimbo la Mkuranga mkoani Pwani mwaka 2020 kupitia Chama cha ACT Wazalendo, Mhandisi Mohamed Mtambo amechangia fedha taslimu ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Dondo.
Mhandishi Mtambo alitoa msaada huo baada ya kuombwa na wananchi wa Kijiji cha Dondo, Kata ya Dondo Tarafa ya Kisiju Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani mwishoni mwa wiki iliyopita akiwa kwenye ziara ya kushukuru wananchi kwa kumpigia kura nyingi katika Uchaguzi Mkuu wa 2020.
Amesema suala la kuchangia, kuhamasisha maendeleo lisihusishwe na itikadi zozote za kisiasa kwa sababu changamoto za wananchi hususan suala la matibabu halichagui nani ataugua na wakati gani.
” Nimekuja hapa kuwashukuru kwa kunipigia kura mwaka jana 2020, nimeona si haki kuwakimbia kwakuwa hatukushinda, nialikeni kwa shughuli zozote za kijamii zikiwemo hitima, harusi, hata kuchimba mitaro ya ujenzi wa zahanati yetu nitakuja.
“Uzalendo kama lilivyo jina la chama chetu ni pamoja na kurudi kutoa shukrani, kuishi na watu kidugu, kuwaunganisha na si kuwagawa hivyo ninatoa kiasi cha Sh.500,000 kuchangia ujenzi wa Zahanati” amesema Mhandisi Mtambo.
Akipokea sehemu ya mchango huo kwa niaba ya Kamati ya Ujenzi wa Zahanati hiyo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Dondo Omary Matope, amesema Kata hiyo haijawahi kuwa na zahanati tangu Tanzania ipate uhuru wake mwaka 1961.
Amesema licha ya Kata hiyo kuwa na idadi kubwa ya watu, shule moja ya msingi na sekondari wamekuwa wakifuata matibabu kwenye kata zingine ambazo zipo umbali mrefu na kijiji chao.
Matope alishukuru mchango huo wa fedha na kuongeza utawasaidia kwenye ujenzi huo wa zahati.
“Hadi sasa wananchi kwa nguvu zetu tumeweza kufyatua tofari 2800 huku mahitaji yakiwa ni tofari 10500 hadi kukamilisha boma lote…., kwa niaba ya wananchi wa Dondo namshukuru huyu kijana wetu kwa kutushika mkono, ni rai yangu niombe wengine waige mfano huu wa kujitoa kwa ajili ya wengine.
“Kama mwenyewe alivyosema, maendeleo hayana chama, kwanza huu si muda wa kampeni, hatuna uchaguzi wowote hapa bali Dondo, kijana wetu ameguswa na changamoto hii kama mtanzania yeyote na si vinginevyo ” amesema Matope.




Discussion about this post