DUNIA huadhimisha siku ya Kasa kila ifikapo Juni 16 ya kila mwaka lengo kuu likiwa ni kuwalinda na kuwatunza kutokana na viumbe hao kuliwa na binadamu licha ya kuwa na umuhimu mkubwa kwa viumbe wengine wa baharini.
Kutangazwa kwa siku hiyo kunatokana na umuhimu wa viumbe hao baharini ambapo pia wamekuwa wakipungua kutokana na kuliwa na binadamu ili hali wanasumu katika miili yao inayotokana na vyakula wanavyokula.
Kasa ni moja kati ya mamilioni ya viumbe wa ajabu wanaoishi baharini ambapo kwa upande mwingine unaweza kusema ni Kobe anayeishi majini.
Kimaumbile kasa anatajwa kuwa katika kundi la reptilia ambaye yupo katika kundi moja na jamii ya Mjusi,Kenge,Mamba na Nyoka ambao hutaga mayai.
Ifahamike kuwa kasa sio samaki lakini ni kiumbe anayeishi baharini na kimaumbile anafafana na Kobe lakini rofauti yao ni kwamba Kasa hawezi kuingiza kichwa wala miguu ndani ya jumba lake kama anavyofanya Kobe pindi anapoona usalama wa maisha yake uko hatarini hivyo hutumia jumba lake gumu kama kinga yake.
Pamoja na kwamba kasa hajulikani na watu wengi duniani lakini maeneo mengi ya pwani pembezoni mwa bahari anafahamika kutokana na kuwa na tabia ya kila anapotaka kutaga mayai yake basi lazima atoke nchi kavu na kuchimba chini kisha akimaliza hufukia na kurudi baharini.
Licha ya kuwa hajulikani sana lakini wakazi wengi wa maeneo ya pwani hasa yenye shughuli za uvuvi humtumia Kasa kama kitoweo bila kufahamu umuhimu wake hali iliyosababisha kuanza kutoweka katika maeneo mengi duniani.

Kasa akiwa baharini(Picha na mtandao)
Shirika la kimataifa la International Union for Convetion Nature (IUCN) liliamua kuikumbusha dunia kuwa licha ya kupigania kulindwa kwa mazingira yote lakini kuna suala la kupotea kwa aina fulani za wanyama,samaki na viumbe wengine wanaoishi majini na nchi kavu kutokana na uchafuzi wa mazingira ya bahari au nchi kavu.
Moja kati ya viumbe vilivyoorodheshwa na IUCN kuwa viko katika hatari ya kutoweka kabisa duniani kwa upande wa baharini ni pamoja na Kasa,Nguva,Potwe na Pomboo ambao hawa wote walikuwa wanapatikana katika mazingira ya bahari ya hindi katika eneo la Tanzania kabla ya wengine kuanza kupotea kabisa hadi sasa.
Kutokana na taarifa hiyo Shirika lisilo la Kiserikali la Sea Sense liliamua kujikita katika kuhamasisha jamii kutunza mazingira ya bahari na kutoa elimu ya umuhimu wa Kasa katika maeneo yao
Mbali na hilo Sea Sense pia ilijikita katika kuhakikisha kuwa fukwe zote zinafanyiwa usafi ikiwemo kuondoa taka za plastiki ambazo viumbe wengi wa bahari hudhani kuwa ni chakula hivyo wanapokula huanza kuathirika.
Sea Sense iliamua kujikita kwa jamii inayoishi mwambao wa pwani kutokana na uwepo wa suala la uvuvi haramu kwa kutumia nyavu ambazo huondoa mazalia ya samaki,kutumia sumu kuvulia samaki na kula baadhi ya viumbe vya baharini kama Kasa ambaye inadaiwa kuwa maeneo walipo viumbe hao ndipo kunapopatikana samaki wengi.

Mtaalamu wa uhifadhi wa mazingira ya bahari na viumbe vyake Omary Mapoy anasema kuna aina tano za Kasa ambazo Kasa Kawaida,Kasa Ng’amba,Kasa Kigome,Kasa Duvi na Kasa Noa
Anasema Kasa Noa ndio Kasa mkubwa zaidi duniani ambaye hukua hadi kufikia uzito wa tani moja lakini wengi hawapo katika maji ya bahari ya Tanzania lakini hutumia baadhi ya sehemu kama malisho yao ya chakula.
Anasema kwa Tanzania Kasa wanaoliwa kwa wingi ni Kasa Kawaida na Kasa Ng’amba ambao ndio hupatika sana katika maji ya bahari ya Tanzania kuliko aina nyingine ya Kasa.
Mapoy anasema Kasa huishi majini pekee lakini Kasa jike ndio hutoka nchi kavu kwa ajili ya kutaga na hutaga mara tano hadi nane kwa mwaka ambapo wao huita (viota) lakini baada ya hapo hukaa miaka miwili ndipo hurudi tena kutaga katika eneo lile lile alilozaliwa.
Anasema Kasa hana tabia ya kusahau alipozaliwa ambapo husafiri umbali mrefu sana kwa ajili ya malisho yao ikiwemo kufika Somalia au Msumbiji lakini akitaka kutaga basi lazima arudi katika eneo alilozaliwa.
Anasema wao wameshafanya utafiti ambao huwafunga kifaa maalum kinachorekodi taarifa zao ikiwemo njia wanazopita na maeneo wanayopendelea kula ambacho kimesaidia sana kugundua malisho ya chakula chao na maeneo wanayopenda kwenda.
“Katika utafiti wetu tuligundua kuwa Kasa anaweza kutoka Mafia hadi Somalia na kurudi tena eneo lilelile kwani tuliwahi kuwafunga Kasa 10 kifaa hicho kwa Kasa wanaotaga Tanzania kwa kuwa wengine hawatagi Tanzania lakini hutumia kama sehemu ya malisho yao na hapo ndipo tulipogundua kuwa Kasa wawili walisafiri umbali wa kilomita 32,000 hadi Somalia na kisha kurudi baada ya miaka miwili kutaga”anasema Mapoy
Mapoy anabainisha kuwa baada ya kutaga huchukua mayai yake na kuhifadhi sehemu maalumu zilizotengenezwa kwa ajili ya usalama zaidi kwa kuwa watu hula mayai yake na hukaa siku 50 hadi 60 kabla ya kutotoa na hali hiyo hutokea kulingana na hali ya hewa.
Anasema baada ya kutotolewa watoto wa Kasa hupelekwa baharini kuendelea na maisha yao hadi wanapofikisha umri mkubwa wa miaka 11 ambapo wakati wote huishi katika maji ya kina kirefu kama sehemu ya usalama wa maisha yao dhidi ya maadui.
Anasema Kasa wanakabiliwa na changamoto kubwa katika maeneo mengi ikiwemo kuliwa na kuvuliwa kwa kutumia sumu.
Anasema uvuvi haramu wa kutumia nyavu za makokoro,sumu,baruti(mabomu) na ukosefu wa elimu juu ya kiumbe huyo ni moja ya sababu kubwa ya kutoweka kwa Kasa licha ya kuwa na sumu kali katika miili yao.
Anasema wavuvi wakishindwa kumvua basi humtegea pindi Kasa jike anapotoka ndani ya maji kwenda katika fukwe za bahari kwa ajili ya kutaga hivyo humkamata na kumchinja kwa kuwa anaweza kufika hadi kilo 350.
“Kwa kuwa Kasa anakula mimea yenye sumu basi wavuvi hutumia njia kadhaa ili kuipima nyama yake kama ina sumu au haina sumu na moja ya njia wanayotumika ni kujipaka damu yake kwenye ngozi na endapo ngozi itawasha basi watajua kuwa nyama hiyo ina sumu na haifai kuliwa”anasema Mapoy Mapoy anaeleza kuwa njia nyingine inayotumika ni kuacha nyama hiyo wazi ili nzi watue na wakishindwa kuruka basi huamini nyama hiyo ina sumu.
Aidha amefafanua kuwa njia nyingine wanaotumia ni kuwapa mbwa au paka vipande vya nyama hiyo na wakiona mbwa wanaendelea kuishi basi nao huamini kuwa nyama hiyo ni safi.
“Wavuvi hawa huhatarisha zaidi familia zao kwani njia nyingine wanayotumia ni kuipeleka nyumbani nyama hiyo na kuruhusu familia zao kuila kabla ya wao kula au kuwagawia majirani kabla ya wao kuanza kuila na wakiona watu wamekufa ndio na wao huacha kula”anasema Mapoy
Mapoy anaongeza kuwa njia hiyo tayari ilishaleta madhara makubwa kwa kusababisha vifo kwa kula nyama ya Kasa ambapo kuna mvuvi alipoteza familia ya mama na watoto wake kwa kula nyama ya Kasa.
Mapoy anabainisha kuwa elimu ni muhimu kwa watu wanaoishi pembeni mwa bahari kwa kuwa Kasa anaweza kusababisha vifo vingi kwa wakati mmoja ikiwa watu watakula nyama yake.
Hata hivyo nyama ya kasa inaonekana kuwa hatari kwa maisha ya binadamu na inawezekana watu wengi wanakufa bila kutangazwa kutokana na kula nyama ya kiumbe huyo katika maeneo mengi ya mwambao wa bahari.
Mwandishi
Goodluck Hongo



Discussion about this post