UGONJWA wa Matende na Mabusha bado haujatokomezwa ambapo kiwango cha maambukizi katika Wilaya ya Kilwa mkoani Lindi kiko juu.
Hayo yamebainishwa mwishoni mwa wiki na Waziri wa Afya Ummy Mwalimu wakati akitoa taarifa juu ya ugonjwa na Matende na Mabusha.
Kwa mujibu wa Ripoti ya Shirika la Afya Duniani (WHO) iliyotolewa Septemba mosi,2013 imeeleza kuwa zaidi ya watu milioni 120 duniani kote wameathiriwa na ugonjwa huo wa mabusha na matende na asilimia 65 ya watu hao wanaishi Kusini Mashariki mwa Asia, wakati asilimia 30 wako barani Afrika na idadi iliyosalia iko katika eneo la tropiki.
Waziri Ummy amesema Mabusha huathiri jinsia zote ingawa kwa asilimia kubwa wanaume ndio wahanga wakubwa.
Hata hivyo wanawake nao hupata Mabusha kwa kiwango kidogo na ili kuweza kuwatofautisha na wanaume ,mabusha kwa wanawake hutambulishwa kwa jina la matende ya sehemu za siri.
Mbali na hilo lakini pia mambukizi ya vimelea vya ugonjwa wa Matende na Mabusha hutokea kwa jinsia zote ,hivyo hata athari zake hutokea kwa jinsia zote.
“Kwa mujibu wa tathmini iliyofanyika mwaka 2018 kwa kushirikiana na Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NMRI) kupitia mradi wa TakeoFF(Tracking Obstacles to Fight Filariasis) katika Wilaya ya Kilwa,wagonjwa wapatao 1,904 walioathirika na matende na mabusha walitambulika.
“Kati ya hao,wagonjwa 1,143 ambayo ni sawa na asilimia 60 ni wale walioathirika na mabusha tu.
“Wagonjwa 697 ambayo ni sawa na asilimia 36.6 ni wale walioathirika na matende tu,na tathmini ilionesha kuwa asilimia 60 ya wagonjwa hao walioathirika na ugonjwa wa matende ni wanawake,na asilimia 4.4 ni wale walioathirika na matende na mabusha kwa pamoja”ameeleza Waziri Ummy
Waziri Ummy ameongeza kuwa katika utafiti huo hakuna mwanamke aliyetambuliwa kuwa na matende ya sehemu za siri.
“Katika Wilaya ya Kilwa mpaka mwaka 2022 jumla ya wagonjwa 547 wa mabusha wamekwishapata huduma ya upasuaji wa mabusha na wagonjwa takribani 1,000 wa matende wamepewa mafunzo ya jinsi ya kujihudumia hususani kutunza usafi wa matende”alisema Waziri Ummy
Hata hivyo Waziri Ummy alibainisha kuwa ugonjwa huo unasababishwa na vimelea vya minyoo wadogo wanaoitwa MICROFILARIA wanaosambazwa na mbu
“Microfilaria hao huenda kuishi kwenye tezi(mitoki) na kuanza kushambulia mfumo wa majidamu(Lymphatic system) ambapo ndio tunatapa jina la kitaalamu la ugonjwa huu kuwa ni Lymphatic Filariasis”alisema Waziri Ummy.
mwisho




Discussion about this post