WADAU wa habari nchini wamependekeza kufanyiwa mapendekezo baadhi ya vifungu vya Sheria ya Huduma ya Habari ya mwaka 2016 na ya Makosa Mtandaoni ya mwaka 2015 kutokana na kutoa uhuru mkubwa waliopewa wasimaizi wa sheria.
Hata hivyo moja ya maeneo yanayoleta mkanganyiko katika Sheria ya Huduma ya Habari ya mwaka 2016 ni kuzuia kutoa taarifa za wawekezaji.
Akifafanua kuhusu changamoto za sheria hizo kwa waandishi wa habari mwishoni mwa wiki,Makamu Mwenyekiti wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika (MISA-TAN) James Marenga amesema licha ya baadhi ya kanuni kuwa zinaleta unafuu lakini asilimia kubwa ni sheria kandamizi.
Amesema baadhi ya vipengele katika Sheria ya Huduma ya Habari ya mwaka 2016 inaunda mahakama ndogo dhidi ya taarifa za waandishi wa habari licha ya kutambua taaluma za wanahabari.
“Kwa mujibu wa Sheria hii kila mwandishi atakuwa na namba maalum lakini Kifungu cha 52(1) kinaelezea suala la uchochezi bila kufafanuwa jambo linaloweza kutumika vibaya na wasimamizi wa sheria”amesema Marenga
Marenga ambaye ni Wakili amefafanuwa kuwa Sheria ya Makosa Mtandaoni ya mwaka 2015 ina vifungu hatari ikiwa haitafanyiwa marekebisho.
Aidha amebainisha kuwa sheria hiyo ilitungwa kwa hati ya dharula na ilitumia siku mbili tu kupitishwa na hakukuwa na waandishi walioshirikishwa katika utungwaji wa sheria hiyo.
“Kifungu cha 50(1) (3)(a)(b)(c) kinaondoa haki ya mtu kukata rufaa hivyo sisi tunapendekeza kuwa haki ya mtu kukata rufaa ni haki ya kikatiba”amesema Marenga.
Marenga ameongeza kuwa wao kama wadau wa habari wanapendekeza pia kuwa kuna maeneo ambayo wao wameyaanisha na kuona kuwa hayo ndiyo yanavunja Katiba na haki za msingi za kupata habari.
Hata hivyo Sheria hizo zimeonekana kulalamikiwa na wadau wa habari na kuitaka serikali kubadilisha baadhi ya vifungu hivyo ili kuzifanya sheria hizo kuwa za kidemokrasia zaidi kama zilivyo baadhi ya nchi barani Afrika ikiwemo Ghana.
Mwandishi:Goodluck Hongo



Discussion about this post