NA MWANDISHI WETU
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan itahakikisha inaendelea kusimamia madai ya madereva pamoja na haki za waajiri katika kutekeleza madai ya madereva wa malori.
Majaliwa ameyasema hayo jijini Dodoma jana (Julai 26, 2022) wakati akizungumza na mawaziri akiwemo Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Prof. Joyce Ndalichako, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, Innocent Bashungwa, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi pamoja na Makatibu Wakuu wa Wizara hizo na Kamishna Jenerali wa Polisi, Camilius Wambura.
“Lengo ni kuhakikisha madereva wanaendelea na ajira zao na wanapata maslahi yao kwa mujibu wa sheria ili waweze kuendesha shughuli zao na familia zao na Serikali itasimamia madai yao na haki za waajiri katika kutekeleza madai ya madereva wasije wakawajibika na vitu ambavyo haviko kwenye sheria zetu za nchi.”alisema Majaliwa
Hata hivyo Waziri Mkuu Majaliwa ametumia fursa hiyo kukitaka Chama Cha Madereva nchini kiruhusu huduma za usafirishaji ziendelee kutolewa wakati Serikali ikiendelea kushughulikia masuala yao.
“Serikali haitaridhika kuona madereva wanalalamika kila siku na pia si vizuri waajiri wakabebeshwa mizigo iliyo nje ya sharia”Amesema Majaliwa
Katika kikao hicho ambacho pamoja na mambo mengine kililenga kujadili suala la mgomo wa madereva wa malori, Majaliwa amefafanuwa kuwa awali kulikuwa na malalamiko ya madereva ambapo Serikali ilikutana na wadau wakiwemo waajiri na wamiliki wa maroli na kukubaliana masuala mbalimbali ya kutekeleza.
Aidha amebainisha kuwa malalamiko ya madereva hao ni kutopewa mikataba ya kazi, kutokuwa na uhakika wa matibabu yao na familia zao (bima ya afya) na kutounganishwa katika mifuko ya hifadhi ya jamii ili wawe na uhakika wa kupata mafao baada ya kustaafu ikiwemo kutopatiwa posho mbalimbali pamoja na kupokelea mishahara yao benki badala ya kupewa mikononi.
“Chama cha madereva kiorodheshe kampuni ambazo hazijatekeleza makubaliano baina yao na madereva badala ya kuzuia malori kutoa huduma kwani kufanya hivyo ni uhujumu uchumi.”amesema Majaliwa
Waziri Mkuu Majaliwa ameeleza kuwa Serikali haipendi kuona mgogoro huo ukiendelea na kuathiri shughuli za waajiri ambao wametekeleza majukumu yao, hivyo ameiagiza Wizara ya Mambo ya Ndani iondoe vikundi vinavyozuia madereva hao kutekeleza majukumu yao.
“Sheria zipo wahakikishe zinasimamiwa na hatua zichukuliwe kwa wanaozikiuka.””amesisitiza Waziri Mkuu Majaliwa




Discussion about this post