NA MBARAKA KAMBONA, ARUSHA
WAFUGAJI wanaofanya shughuli zao Kanda ya Kaskazini wameiomba Serikali kuhakikisha Maafisa Ugani wanawafikia ili kuwapatia huduma stahiki ili ufugaji wao uwe bora na wenye tija.
Wakizungunmza kwa nyakati tofauti katika Maonesho ya Wakulima NaneNane Kanda ya Kaskazini yanayofanyika mkoani Arusha leo, Wafugaji hao walisema ni muhimu maafisa ugani kuwatembelea wafugaji kila wakati na kutatua changamoto zinazowakabili.
Mmoja wa wafugaji hao Desderi Kimario amesema wanahitaji maafisa ugani wa Kilimo na Mifugo wote kwa pamoja wawe wanafanya kazi karibu na wafugaji ili wafugaji hao waweze kufanya shughuli zao kwa kuzingatia ushauri wa wataalamu hao na kufanya ufugaji wao uwe na tija na nchi kwa ujumla.
“Tunaomba maafisa ugani wawe wanatutembelea mara kwa mara sisi wafugaji wadogo wadogo katika maeneo yetu huku kwenye Kata na Vijijini ili kujua matatizo yetu na sio mpaka tufike kwenye maonesho kama hivi, kwa sababu maonesho huwa ni mara moja kwa kila mwaka”, amesema Kimario Nayen Lawrence Kimambi, mfugaji kutoka mkoani Kilimanjaro amesema kwa sasa ardhi imekuwa finyu hivyo ni muhimu wafugaji wakaendelea kupatiwa elimu ya kulima malisho ya mifugo ili kuokoa changamoto ya malisho na kuleta manufaa zaidi kwa jamii za wafugaji na nchi kwa ujumla.
Kwa upande wake Kevin Manase kutoka Arusha amesema kuwa kama wafugaji wataendelea kuelimishwa vizuri kuhusu umuhimu wa ulimaji wa malisho ya mifugo basi sio muda mrefu migogoro kati ya wakulima na wafugaji itakwisha.
Kwa Upande wake, Afisa Mifugo Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo, Israel Kilonzo aliwashauri wafugaji hao kuanza kujifunza namna ya kustawisha malisho ya mifugo na kuachana na tabia ya kutegemea malisho ya asili peke yake kwani kufanya hivyo kutasaidia kupunguza migogoro ya ardhi.
“Kama tunavyojua watu wanaongezeka na mifugo pia inaongezeka na ardhi iliyopo haitoshi kufanya ufugaji wa kuhamahama, ni lazima tujifunze kustawisha malisho katika maeneo yetu na tujifunze kuyatumia vizuri ikiwemo kuwa na mifugo tutakayoimudu kuihudumia”, amesema Kilonzo




Discussion about this post