NA MWANDISHI WETU, MAGU
NAIBU Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja amesema amewataka wananchi kuwa wazalendo katika kulinda vitalu vya miti ili kuhifadhi mazingira.
Masanja ametoa kauli hiyo leo wilayani Magu mkoani Mwanza wakati akikagua mradi wa kitalu cha miche ya miti wenye thamani ya Sh.Milioni 43 unaotekelezwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) .
Amesema ni muhimu kwa wananchi kuwa wazalendo kwa kuitunza miche ya miti watakayokabidhiwa na TFS ili iweze kuleta matokeo chanya ya kuhifadhi mazingira.
“Tuwaombe wananchi miche hii watakapogawiwa waitunze vizuri kwa ajili ya vizazi vya sasa na vizazi vijavyo”amesema Masanja
Ameongeza kuwa katika utekelezaji wa mradi huo, awamu ya kwanza zimetolewa fedha kiasi cha Sh.Milioni 17 kwa TFS ambapo Serikali itaendelea kutoa fedha kwa awamu nyingine ili kukamilisha mradi.
Ameongeza kuwa lengo la uanzishwaji wa kitalu hicho ni kupunguza athari za uharibifu wa mazingira hususan katika Mkoa wa Mwanza ambapo kwa sasa utekelezaji wake umeanzia Wilaya ya Magu.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Magu Salum Kali amesema kupitia kitalu hicho wananchi wa Wilaya ya Magu watanufaika sana kwa sababu miche itapelekwa kwenye maeneo ambayo yalikwishaharibika ili kuyarudisha kwenye asili yake ya awali.
Aidha Kali amewataka wananchi kuitunza na kuilinda miche ya miti watakayokabidhiwa .
“Kila mwananchi awe mlinzi wa mwenzake na kwa wale wafugaji msiingize mifugo kwenye maeneo ambayo tumepanda miti”amebainisha Kali

Kwa upande wake Kaimu Kamanda wa TFS Kanda ya Ziwa, Thomas Moshi amesema kitalu hicho kitakuwa na uwezo wa kuzalisha miche laki tatu kwa mwaka, hivyo kuendelea kuihudumia jamii ili kuhakikisha maeneo ambayo hayana miti na uoto wa asili unarudi.
Aidha amefafanuwa kuwa wananchi wanatakiwa kuelimishwa ili waweze kujua faida za miti katika kuleta nishati mbadala, kuleta mvua na pia kutumika kama mitishamba ya dawa za asili.
Kitalu hicho kimefadhiliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii chini ya Mfuko wa Misitu Tanzania (Taff kwa kushirikiana na TFS.




Discussion about this post