NA MWANDISHI WETU
HALMASHAURI nchini zimeombwa kutenga fedha za mikopo isiyo na riba kwa Wazee ambao wanakabiliwa na hali ngumu ya maisha kutokana na kupanda kwa gharama za maisha.
Wito huo umetolewa Chanika jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki na Mwenyekiti wa Taasisi isiyo ya kiserikali ya Jai Juma Mwaipopo wakati wa maadhimisho ya siku ya Wazee duniani .
Mwaipopo ambaye amesema hali ya Wazee ni mbaya licha ya kuwa wao ndio waliofanisha maendeleo yanayoonekana sasa.
Amesema Wazee ni hazina ambapo ndani yao kuwa madaktari, wahandisi, mafundi na wenye fani mbalimbali ambao wakikaa pamoja wanaweza kuunda kitu kinachoweza kuwaingizia kipato kutokana na kiwango kidogo wanachopata baadhi yao cha malipo ya uzeeni (Pesheni).
“Nilikuwa Diwani wa Kata ya Ukonga na wakati nilipokuwa hapa niliona jinsi Wazee wanavyotaabika hivyo nilifanikiwa kuanzisha Umoja wao lakini pia nilipofika Zingiziwa kutoa msaada niliambiwa kuna mzee alifariki kwa kula udongo kutokana na njaa.
“Nilihuzunika sana sasa kama mjini wazee wako hivi huko mikoani hali ikoje hivyo mimi ninashauri Halmashauri zote nchini zitenge fedha kwa ajili ya kuwasaidia wazee kama wanavyofanya kwa Watu wenye ulemavu, Wanawake na Vijana”amesema Mwaipopo.
Mwaipopo ameongeza kuwa licha ya Serikali kuwa na mpango wa TASAF wa kusaidia Kaya masikini lakini walengwa hawafikiwi na fedha hizo wakiwemo Wazee hivyo kunahitajika mikakati ya kuwasaidia Wazee.
“Wazee sasa hivi ndio wameachiwa mzigo mkubwa wa familia kutokana na vijana wao wengi kukosa ajira hivyo wengi wao wanapokea Sh.100,000 na chini ya hapo hivyo hawawezi kupambana na hali ya maisha ya sasa,ni muhimu kwa Serikali kuwaongezea fedha kama wanavyofanya kwa watumishi wengine wanaoongezwa mshahara”amebainisha Mwaipopo

Mwaipopo akiongozana na viongozi wa Jai walifanikiwa kutoa misaada mbalimbali kwa Wazee wa Kata ya Zingiziwa kwa kuwapatia vyakula mbalimbali ikiwemo mchele, sukari sabuni ambavyo vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya Sh.600,000




Discussion about this post