NA MWANDISHI WETU
KATIBU Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Mary Maganga amesema Serikali imeandaa Mpango wa Kitaifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira ambao utatekelezwa kwa kipindi cha miaka 10
Amesema mpango huo utaainisha changamoto za kimazingira na mikakati ya kukabiliana nazo kwa kuzingatia utofauti wa maeneo mbalimbali.
Maganga ameyasema haya leo Oktoba 13, 2022 jijini Dar es Salaam katika Mkutano kati ya Ofisi ya Makamu wa Rais na Washirika wa Maendeleo.
Ameongeza kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais imeona ni busara kuitisha mkutano huo kwa nia ya kushirikisha wadau hao wa maendeleo,jitihada ambazo Serikali inafanya na kuainisha maeneo ambayo wanahitaji kushirikiana nao kwa karibu zaidi hasa katika maeneo yenye changamoto za mazingira kwa kutumia Mpango Kabambe wa Kitaifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira.
Aisha Maganga amebainisha kuwa mkutano huo utatumika kuweka mikakati ya kupanga, kufadhili na kutekeleza afua za kimkakati ili kutatua changamoto zilizoainishwa na kuendeleza ushirikiano wa muda mrefu katika maeneo ya uhifadhi na usimamizi wa mazingira kati ya Serikali na wadau wa Maendeleo.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Amina Khamis Shaban alipongeza Ofisi ya Makamu wa Rais kwa jitihada zake katika kusimamia uhifadhi wa mazingira.
Amesema kuzinduliwa kwa Mpango Kabambe wa Mazingira ni hatua ambayo itachochea katika kupata fedha za kusaidia katika hifadhi ya mazingira.
“Hata hivyo, Serikali inaendelea kujipanga kuhakikisha changamato za kimazingira zinatatuliwa kwa kupanga bajeti kupitia wizara zake,” amesema Shaban.
Kwa upande, Mwakilishi mkazi wa Umoja wa Mataifa na Mwenyekiti wa Kundi la washirika wa Maendeleo nchini (Development Partners Group on Environment, DPG) Zlatan Milisic amesema kwa kushirikiana na wadau wenzake wako tayari kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha utekelezaji wa Mpango Kabambe wa Kitaifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (2022-2023)
Mpango Kabambe wa Taifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira umeainisha changamoto 12 za mazingira zinazoikabili nchi ikiwa ni pamoja na uharibifu wa ardhi, uharibifu wa vyanzo vya maji, athari za mabadiliko ya tabianchi, uchafuzi wa mazingira, ukataji hovyo wa miti na uharibifu wa misitu.
Changamoto zingine ni upotevu wa makazi ya wanyamapori na bioanuai, uharibifu wa mfumo-ikolojia ya pwani na baharini, uharibifu wa ardhi oevu, usimamizi hafifu wa taka, kuenea kwa viumbe vamizi, na changamoto za mazingira katika miji.
Ili kupata ufumbuzi wa changamoto hizo Mpango huo umeainisha hatua za kimkakati na mahsusi kwa kuzingatia jiografia na mifumo ikolojia ya maeneo husika.




Discussion about this post