NA GOODLUCK HONGO
MWENYEKITI wa Taasisi isiyo ya kiserikali ya Jai Juma Mwipopo ameitaka Serikali kuangalia gharama za matibabu ya figo ili kusaidia watu wenye kipato cha chini kupata huduma hiyo.
Mwaipopo ambaye ni Diwani Mstaafu wa Kata ya Ukonga kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ametoa wito huo baada ya kutembelea wajane,wagonjwa na wazee wakiwemo wasiojiweza katika maeneo mbalimbali ya Kata hiyo kwa lengo la kuwapatia misaada ili kujikimu na hali ya maisha
Akizungumza jijini Dar es Salaam leo Oktoba 23,2022 wakati wa ziara ya kutembelea wagonjwa katika Kata ya Ukonga, Mwaipopo amesema ni muhimu kwa Seikali na wadau wengine wa Sekta ya Afya nchini kuangalia na kusaidia kupunguzwa kwa gharama za matibabu ya ugonjwa wa figo ili kusaidia kundi la watu wasio na uwezo kumudu gharama hizo.
“Nipo hapa leo nipo Mtaa wa Sabasaba na Kichangani nikiwa na mmoja wa wagonjwa wanaougua figo na matatizo makubwa ya mjane huyu ni kushindwa kupata matibabu ya figo kwa wakati.
“Mama akiwa anaumwa figo mwaka wa tatu sasa akiwa kitandani na tumbo limejaa hana msaada,anashindwa hata kuongea anatakiwa kwa wiki akatolewe maji mara tatu.
“Kila akienda hospitali kupata huduma hiyo lazima awe na Sh .120,000 hivyo kwa wiki anatakiwa awe na zaidi ya Sh.300,000 hali ambayo hawezi kuimudu,lakini kama kungekuwa na ufadhili au matibabu kuwa na gharama ya chini ya ndugu wangesaidia lakini haiwezekani kila wiki awe na fedha hizo”amesema Mwaipopo
Mwaipopo amebainisha kuwa mama huyo ikiwa hajapata matibabu kwa wakati, tumbo huvimba hali inayokatisha tamaa kwa familia hasa kutokana na kushindwa kumudu gharama za matibabu.
“Kwa kweli kama hujaona huwezi kuwa na uchungu lakini inawezekana kuna wagonjwa wengi wa figo wako nyumbani kwa kushindwa kugharamia matibabu ya figo hivyo kupoteza maisha lakini kama serikali iliangalie jambo hili maana gharama ni kubwa sana”ameongeza Mwaipopo
Mwaipopo amekuwa akitembelea mitaa mbalimbali ya Kata hiyo na kutoa misaada mbalimbali vikiwemo vyakula na kusaidia watu wasiojiweza na wale wanaokabiliwa na magonjwa yenye gharama kubwa ili kuwatia moyo na kuchangia gharama zao.





Discussion about this post