NA MWANDISHI WETU,TABORA
NAIBU Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) Dkt. Switbert Mkama amezitaka halmashauri nchini kuipa kipaumbele miradi ya mazingira ili kusaidia kurejesha Ardhi iliyoharibika na kuongeza usalama wa chakula.
Haya hivyo Dkt.Mkama ameonesha kutoridhishwa na usimamizi wa Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na kuongeza usalama wa chakula unaotekelezwa katika Halmashauri ya Nzega mkoani Tabora licha ya kuwa tayari fedha zimeshatolewa na Serikali kwa Halmashauri za wilaya zinazotekeleza miradi hiyo.
Dkt.Mkama ametoa kauli hiyo Oktoba 24,2022 wilayani Nzega Mkoa wa Tabora wakati wa ziara ya kutembelea na kukagua Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo yenye Ukame nchini (LDFS).
Amesema inashangaza kuona namna wilaya inavyotekeleza miradi ya Serikali kwa kutoipatia kipaumbele miradi ya mazingira kama inavyofanya kwa miradi mingine katika wilaya hiyo.
“Matumizi ya fedha katika mradi huu hayaridhishi hata kidogo, kwa mwaka 2022/23 Nzega mmetengewa Sh. Bilioni 2.3 na kati ya hizo Sh.Milioni 467.6 zipo kwenye akaunti bado hazijatumika na mpaka Desemba zinatakiwa ziwe zimetumika hali hii hairidhishi hata kidogo,” amesema Dkt.Mkama
Dkt.Mkama aliutaka uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nzega kujitathmini kuhusu utendaji wake na kutoa siku saba wa kuandaa mpango kazi wa utekelezaji wa kazi hiyo.
“Haiwezekani katika miezi miwili ya mkataba mkandarasi ana siku 23 hajafanya kazi yoyote lakini halmashauri iko kimya, mkurugenzi yuko kimya, mratibu wa mradi wa wilaya yuko kimya hamchukui hatua,” ameongeza Dkt.Mkama
Kutokana na hali hiyo alielekeza kusitishwa kwa mkataba dhidi ya mkandarasi huyo kwani ameshindwa kutekeleza majukumu yake na kuusimamia mkataba wake na halmashauri.
Aidha, katika hatua nyingine alimtaka Mkurugenzi wa halmashauri kumchukulia hatua Afisa Manunuzi kwa kufanya mchakato wa kununua mashine ya kukoboa mpunga kupitia mradi huo ambayo inadaiwa kutokidhi viwango na kutoendana na bei halisi.
Naibu Katibu Mkuu Mkama amebainisha kuwa mashine hiyo inaoekana imetajwa kununuliwa kwa Sh. Milioni 50 tofauti na viwango na kuelekeza Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Ndani wa Serikali ishirikishwe na kupewa kazi ya kuikagua kujua kama inakidhi viwango.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Wilaya ya Nzega Evance Chambo amesema amepokea maelekezo hayo na kuahidi kuwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya itasimamia kikamilifu utekelezaji.
Amesema atamuelekeza mratibu wa mradi wa wilaya awe anatoa taarifa za utekelezaji kila wiki ili kuhakikisha unatekelezwa kama ulivyopanga kuepuka changamoto kama hizo.
Dkt. Mkama na timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais amefanya ziara ya kutembelea na kukagua mradi wa LDFS katika wilaya za Magu (Mwanza), Nzega (Tabora) na Mkalama (Singida) na miradi mingine ikiwemo uchimbaji wa visima virefu vya maji katika kijiji cha Bulende na Bulambukana mradi wa ufugaji nyuki katika kijiji cha Lyamalangwa




Discussion about this post