NA MWANDISHI WETU
CHAMA Cha NCCR-Mageuzi kimesema mchakato wa kupatikana kwa Katiba Mpya si wa chama kimoja bali ni takwa la watanzania wote.
Hata hivyo chama hicho kimeonesha ku shangazwa na wanasiasa wanaokishambulia Kikosi Kazi kilichoundwa na Rais kukusanya maoni ili hali wengine walienda hadi Ikulu kuzungumza na Rais juu ya suala hilo.
Hayo yamezungumzwa leo Oktoba 28 ,2022 Makao Makuu ya chama hicho jijini Dar es Salaam na Makamu Mwenyekiti Bara Joseph Selasini wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Selasini amesema mchakato wa kudai Katiba Mpya ulianza mwaka 1991 ndani ya chama hicho na ndio sababu ya kuitwa NCCR-Mageuzi hivyo ni wao ndio wanaopaswa kusema waanzilishi wa mchakato huo lakini baadhi ya vyama na watu wengine wamekuwa wakijiona kuwa wao ndio wenye haki na sababu ya kufanyika mchakato huo jambo ambalo si la kweli.
“Rais alikubali mwenyewe kuunda Kikosi Kazi kama wengine walivyounda Tume kama za Jaji Kisanga,Jaji Nyalali na Jaji Warioba ambapo wengine walizunguka nchi nzima na wengine walikusanya maoni ya wachache lakini watanzania wanashawishiwa juu ya Tume ya Jaji Warioba kuwa na maoni bora, ni sawa lakini hatupaswi kuibeza kazi ya Kikosi Kazi.
“Nyinyi mlienda Ikulu kutoa maoni yenu hivyo na wale ambao hawajaenda Ikulu walikwenda kwenye Kikosi Kazi na vyama vingine viliitwa hadi kwenye mkutano wa maridhiano lakini hao hao ndio wanaona kuwa waliokwenda kutoa maoni kwenye Kikosi Kazi hawakuwa sawa jambo ambalo si la kweli.
“Hata sisi NCCR-Mageuzi tulitamani kwenda Ikulu kuzungumza na Rais lakini hatukupata nafasi wala kutoa maoni yetu kwa sababu ya migogoro ya uongozi ndani ya chama chetu,hivyo mimi naamini maoni yote ya Kikosi Kazi na wale waliokwenda Ikulu yatajumuishwa pamoja la muhimu ni kumpa muda Rais”amesema Selasini
Selasini ameongeza kuwa mchakato huo umepitia hatua nyingi ukihusisha Tume ya Jaji Nyalali,Kisanga,Warioba na sasa Kikosi Kazi hivyo kukishambulia ni makosa na jambo muhimu ni kuchambua ili kuendelea na mchakato huo kwa kuwa Rais ameonesha nia njema tofauti na viongozi wengine.
“Rais hawezi kuwaita viongozi wa upinzani Ikulu kunywa juisi bali walikwenda kuzungumzia masuala muhimu ya nchi kama Katiba Mpya,Mikutano ya Vyama vya Siasa na masuala muhimu kwa Taifa lakini kama wanasiasa wasipokuwa makini watasababisha kutopatikana kwa jambo hilo”ameeleza Selasini
Selasini amefafanua kuwa Serikali ya Awamu ya Tano haikutaka kuruhusu mijadala ya Katiba Mpya na hakukuwa na mtu yeyote aliyethubutu kuzungumzia hilo lakini Serikali ya Awamu ya Sita imetoa fursa hiyo ili kuwe na muafaka wa kitaifa na watu wabaki na furaha katika nchi yao
“Wanasiasa hawa hawa ndio waliosababisha kuvunjika kwa Bunge Maalum la Katiba na mimi nilikuwepo lakini naamini kama tungefikia mwisho basi tungepata hata kidogo kuliko kuishia kati lakini waliosababisha ni wanasiasa”amesema Selasini
Hata hivyo Selasin amemuomba Rais Samia Suluhu Hassan kuwa yale yanayowezekana kutekelezwa kwa sasa yafanyiwe kazi mapema kwa kuwa 2024 wana uchaguzi ili waanze kufanya mikutano ya hadhara”amesema Selasin
Akizungumzia kuhusu mgogoro wa uongozi ndani ya chama hicho,Selasin ameongeza kuwa kazi walishamaliza Dodoma na kwamba sheria inawataka vikao vyote vikubaliwe na Ofisi ya Msajili na hivyo wameshafanya hivyo.
“Tuna barua hii hapa kutoka Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ambaye ameridhia vikao vyote tulivyofanya na maamuzi yaliyochukuliwa sasa hao wengine wanaozungumza nje kuwa ni viongozi wa NCCR-Mageuzi tunaomba hatua zichukuliwe.
“Tukiitwa mahakamani tutaenda lakini kwa sasa tunaomba IGP na Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua wote wanaojitangaza kuwa ni viongozi wa chama chetu wakati hapa Makao Makuu hawajulikani wala kutambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa”amebainisha Selasini




Discussion about this post