NA GOODLUCK HONGO
SHIRIKA la Kimataifa la Amref Health Africa limetoa kiasi cha dola za kimarekani Milioni 1.9 kwa nchi nne za Afrika ili kuimarisha mifumo ya afya katika ngazi ya wilaya. Lengo la kutolewa kwa fedha hizo ni kusaidia mipango ya kuimarisha mifumo ya afya katika ngazi ya wilaya kote katika nchi nne za Afrika ikiwemo Tanzania, Uganda, Kenya na Malawi
Kwa mujibu wa taarifa kutoka Shirika la Global Health Strategies kwa niaba ya AMREF iliyotolewa leo Oktoba 25,2022 jijini Nairobi,Kenya imeeleza kuwa Shirika hilo litakabidhi Dola za Marekani Milioni 1.9 kama ruzuku ndogo kwa mashirika tisa ya Kiafrika yasiyo ya kiserikali.
Taarifa hiyo imebainisha kuwa Mashirika yasiyo ya kiserikali yatashirikiana na Amref kutekeleza mikakati ya ndani ya kuboresha utoaji wa Chanjo dhidi ya Ugonjwa wa UVIKO-19 miongoni mwa watu walio katika hatari kubwa hadi mwisho wa 2023.
“Maendeleo haya yanatokana na majadiliano yaliyoongozwa na Mtandao wa Chanjo (VAN), mpango wa kujifunza kati ya viongozi wa afya katika Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara ili kuboresha kampeni za chanjo nchini kote na kuongeza upokeaji wa Chanjo dhidi ya UVIKO-19”ilieleza taarifa hiyo.
Akizungumzia kuhusu fedha hizo,Meneja wa Mradi, Kitengo cha Usalama wa Afya Ulimwenguni katika Amref Health Africa Jackson Musembi alisema fedha hizo ni sharti watafute njia za kuongeza juhudi za kupambana na ugonjwa huo huku wakijenga upya kinga zao dhidi ya magonjwa mengine ya kuambukiza kupitia kuimarisha mifumo ya afya katika viwango vyote.
“Kupitia VAN, washirika wengine walio Afrika Mashariki na Kusini wanafanya kazi katika mipaka yote ili kushiriki mikakati iliyotayari kutumika kwa ajili ya utoaji ujumbe na uwasilishaji wake kwa ufanisi,tunajivunia kutoa msaada huu pamoja na washirika wetu kutoka kwa wakfu wa The Rockefeller Foundation.”alisema Musembi
Amref Health Africa ni Shirika la Kimataifa la Kiafrika lililoanzishwa mwaka wa 1957 na Madaktari wa Afrika Mashariki ili kutoa msaada muhimu wa matibabu kwa jamii za mbali za Afrika Mashariki.
Shirika hilo lenye Makao Makuu yake nchini Kenya, ndilo Shirika kubwa zaidi la Kimataifa lisilo la Kiserikali (INGO) lenye makao yake barani Afrika likiwa na lengo la kuongeza ufikiaji endelevu wa afya.
Amref inaendesha mipango mbalimbali katika nchi 35 barani Afrika, ikiwa imejifunza mambo kwa zaidi ya miaka 60 na kushirikisha Serikali, Jumuiya na Washirika.
Kadhalika, Amref Health Africa inashiriki katika uandaaji wa mipango(programu), uchangishaji, ushirikiano, utetezi, ufuatiliaji na utathmini ambapo pia ina ofisi zake barani Ulaya na Amerika Kaskazini.




Discussion about this post