NA MWANDISHI WETU
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango amewataka wataalamu na wawekezaji kujadili kwa pamoja namna bora ya kutunza, kusimamia na kuwekeza katika rasilimali adhimu za fukwe zilizopo nchini ili kuongeza mchango wake kwenye maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Makamu wa Rais ameyasema hayo leo Novemba 23, 2022 jijini Mwanza wakati akifungua Jukwaa la Nane la Maendeleo Endelevu lenye dhima ya Usimamizi Madhubuti wa Fukwe kwa Maendeleo endelevu.
Amesema unahitajika ubunifu katika kutumia zaidi ya kilomita 1400 za ukanda wa Pwani ya bahari na fukwe safi, hifadhi tatu za baharini,maeneo tengefu ya baharini 15, maziwa na mito mikubwa ambayo kwa pamoja inaongeza idadi kubwa ya fukwe ambazo bado hazijaweza kutumika kikamilifu kwa ajili ya maendeleo ya taifa.
Aidha Dkt Mpango amesema serikali ya awamu ya sita imeweka mkazo katika kuendeleza Uchumi wa Buluu pamoja na suala la hifadhi na usimamizi wa mazingira nchini.
Ameongeza kwamba dhamira ya Serikali ni kuharakisha maendeleo endelevu ya taifa kwa kuzingatia malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 inayolenga kufikia uchumi jumushi wa Taifa lenye kipato cha kati na maisha bora kwa kila Mtanzania.
Mbali na hilo lakini pia pia ameagiza kila Mkoa, kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais – Muungano na Mazingira, pamoja na wadau wengine kujipanga na kuharakisha mchakato wa kuandaa mpango mkakati utakaoainisha namna ya kufanya uwekezaji wa kuendeleza fukwe zilizopo nchini pamoja na bustani za kupumzikia.
Makamu wa Rais amewasihi viongozi wa mikoa kutekeleza suala la upandaji miti kwa ufanisi ikiwemo ufuatiliaji wa miti hiyo kuhakikisha inafanikiwa kukua kama ilivyopangwa na kuweka malengo yanayotekelezeka ikiwemo kuwatumia wakala wa misitu nchini (TFS) katika elimu sahihi ya miti itakatokuwa rafiki wa vyanzo vya maji na mazingira.

Awali akitoa taarifa za kuhusu kongamano hilo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi (Uongozi Institute) Kadari Singo amesema kongamano limelenga kujadili fursa zilizopo katika uwekezaji wa fukwe kama kichochezi cha maendeleo, changamoto zinazohusiana na utunzaji na usimamizi na uwekzaji wa fukwe pamoja na mifumo ya kisera, kisheria na kitaasisi inayohusiana na usimamaizi wa fukwe nchini.
Singo ameelezea dhima ya mwaka huu katika kongamano hilo kuwa inalenga kufungua majadiliano katika kuelekea kupata suluhisho la namna Madhubuti ya kusimamia na kuwekeza katika fukwe za bahari, maziwa na mito nchini ili ziweze kutoa tija katika ukuaji wa uchumi hapa nchini.
“Dhima imezingatia dhamira ya dhati ya serikali inayolenga kuimarisha uchumi wa nchi pasipo kuharibu mazingira”amefafanua Singo




Discussion about this post