LUANDA,ANGOLA
JESHI la Jumuiya ya Afrika Mashariki limewekwa katika hali ya utayari kuyakabili makundi yote ya waasi Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) likiwemo kundi maarufu la M23 ikiwa yatagoma kuweka chini silaha zao ifikapo Novemba 25,2022
Uamuzi huo umetangazwa Novemba 24,2022 nchini Angola mara baada ya kikao kilichoongozwa na Rais wa Angola Joao Lourenco na kuhudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) Felix Tshisekedi, akiwemo Rais wa Burundi Evariste Ndayishimiye na na mjumbe wa amani wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambaye ni Rais wa zamani wa Kenya Uhuru Kenyatta.
Mkutano wa viongozi hao umetoa amri ya kusitishwa mapigano ifikapo Novemba 25,2022 saa 12:00 jioni na makundi yote ya waasi wenye silaha hasa la M23 wanaodai kwamba wanapigania haki za watu kutoka kabila la Watutsi Mashariki mwa DRC, kuondoka katika miji ambayo linashikilia ukiwemo mji wa Bunagana.
Taarifa hiyo aidha imesema, waasi watapewa ulinzi na Jeshi la DRC, Jeshi la Jumuiya ya Afrika Mashariki na wanajeshi wa Umoja wa Mataifa (MONUSCO) endapo watajisalimisha.
Wanajeshi wa Kenya na Burundi tayari wapo nchini DRC huku Uganda ikitarajiwa kutuma wanajeshi 1000 wiki ijayo.
Maamuzi hayo yamekuja siku chache baada ya aliyekuwa Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta kusema kwamba Rais wa Rwanda Paul Kagame, anayetuhumiwa kuunga mkono waasi wa M23, ameahidi kushawishi waasi hao kuacha vita.
Rwanda imewakilishwa kwenye mkutano huwa wa Novemba 23,2022 na Waziri wa Mambo ya Kigeni Vincet Biruta.
Serikali ya Rwanda imekuwa ikituhumiwa na Serikali ya DRC kuwa inawaunga mkono na hata kuwasaidia kijeshi waasi wa M23, tuhuma ambazo Kigali imekuwa ikizikanusha.




Discussion about this post